2013-12-20 13:42:26

Fumbo la Umwilisho linagusa: maskini, uinjilishaji na furaha!


Padre Raniero Cantalamessa, mhubiri wa nyumba ya kipapa katika mahubiri yake ya tatu wakati huu wa Kipindi cha Majilio, amegusia kuhusu Fumbo la Umwilisho mintarafu tafakari iliyofanywa na Mtakatifu Francisko wa Assisi; uhusiano kati ya maskini na Siku kuu ya Noeli; changamoto ya kuwapenda, kuwasaidia na kuwainjilisha maskini. Siku kuu ya Noeli iwe ni kielelezo cha furaha mbinguni na amani duniani.

Mahubiri haya yamehudhuriwa na Baba Mtakatifu Francisko, Makardinali, Maaskofu na wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume. Padre Cantalamessa anasema kwamba, utamaduni wa kutengeneza Pango la Mtoto Yesu umeasisiwa na Mtakatifu Francisko wa Assisi aliyependa kuwaonjesha waamini umaskini ambayo Mtoto Yesu alikumbana nao wakati wa kuzaliwa kwake mjini Bethelehemu: Huyu ndiye Mungu aliyefanyika mwili kwa njia ya Roho Mtakatifu akawa mwanadamu; akajinyenyekesha hata kufa Msalabani; Ni Mungu aliyeonja umaskini wa binadamu.

Kadiri ya Mafundisho ya Mababa wa Kanisa, kuna uhusiano mkubwa kati ya Siku kuu ya Noeli na Maskini wanaonesha unyenyekevu na mateso, kiasi hata cha Yesu mwenyewe kujitambulisha nao! Mwaliko kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwahudumia maskini kwa njia ya matendo ya huruma, kwani kwa kufanya hivi kwa maskini na wadogo, wanamhudumia Kristo mwenyewe! Kanisa halina budi kujitambulisha na Maskini kama alivyowahi kusema Papa Yohane XXIII, wakati wa Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Hii ni kutokana na ukweli kwamba, kwa njia ya sakramenti ya Ubatizo, wanakufa na kufufuka pamoja na Kristo. Waamini na watu wenye mapenzi mema, waguswe na mateso pamoja na mahangaiko ya maskini duniani na kamwe wasiwapatie kisogo. Jamii ijitahidi kujenga na kuimarisha utamaduni wa Injili ya Upendo na Maisha kwa kuwasaidia: wazee, maskini na watoto wanaokumbana na baa la njaa na utapiamlo ili waweze kuwa na uhakika wa maisha ya leo na kesho iliyo bora zaidi kwa kubadili mtindo wa maisha!

Padre Cantalamessa anasema, upendo kwa maskini ni kielelezo cha utakatifu wa maisha kama walivyoonesha watakatifu wengi, kati yao Mtakatifu Vincenti wa Paulo na Mama Theresa wa Calcutta. Utakatifu umekuwa ni njia na karama ya maisha yao ya kitawa.

Maskini waheshimiwe na kuthaminiwa kama binadamu na ndugu zake Yesu, kwani, udugu ni msingi na njia ya amani. Maskini wasaidiwe kupambana na majanga ya maisha kwa njia ya mshikamano wa upendo unaoongozwa na kanuni auni. Kamwe, watu wasizibe maskio kwa kutotaka kusikiliza kilio cha maskini. Jumuiya ya kimataifa iunganishe nguvu zake katika mapambano dhidi ya baa la umaskini wa hali na kipato.

Maskini pia wanapaswa kutangaziwa Habari Njema ya Wokovu! Washirikishwe Neno la Uzima na Mkate ulioshuka kutoka mbinguni; waonjeshwe tone la matumaini kwa leo na kesho iliyo bora zaidi. Maskini wana haki ya kusikia ujumbe mzima wa Injili ukitangazwa kwao.

Kwa Mtakatifu Francisko, Siku kuu ya Noeli ilikuwa ni kielelezo cha kuonesha ile furaha inayobubujika kutoka katika undani wa moyo wa mwamini kwani Mtoto Yesu anakuja kati ya watu wake katika hali ya umaskini, kielelezo cha hali ya juu kabisa cha upendo wa Mungu kwa binadamu. Nyimbo za Noeli zinawaonjesha waamini na watu wenye mapenzi mema furaha ya Noeli.







All the contents on this site are copyrighted ©.