2013-12-20 07:55:47

Chimbuko la haki msingi za binadamu!


Wakristo na uhuru wa kidini ndiyo kauli mbiu ambayo imeongoza semina ya siku moja iliyoandaliwa na Mradi wa uhuru wa kidini kutoka Chuo Kikuu cha Georgetwon pamoja na Kituo cha Masuala ya Kidini cha Berkley, vyote kutoka nchini Marekani. Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican alishiriki katika warsha hii. RealAudioMP3

Anasema, dhana ya uhuru wa kidini ni jambo ambalo limeibuliwa na Kanisa na kushuhudiwa na waamini kiasi hata cha kuyamimina maisha yao kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake kama alivyofanya Mtakatifu Thomas More. Waamini kwa kusukumwa na dhamiri nyofu na akili timamu wanayo haki ya kukataa utawala wa kidhalimu na nyanyaso za kidini. Dhana hii imefundishwa na Yesu mwenyewe na Mtakatifu Paulo anasema, waamini wamekombolewa na Kristo na kwamba, uhuru wa ndani unayo nafasi ya pekee hata katika maisha ya hadhara ndani ya Jamii.

Jumuiya ya Kimataifa Mwaka 2013 inaadhimisha Miaka 1700 tangu Azimio la Milano lilipopitishwa na hivyo kutoa haki ya kuwa na uhuru wa mtu kuabudu dini anayotaka. Uhuru wa kidini ni chimbuko la tamaduni na urithi mkubwa wa maisha ya binadamu, mahusiano na mshikamano kati ya watu wa mataifa na dini mbali mbali. Uhuru wa kidini ni dhana inayopaswa kuangaliwa kwa makini kwani inaweza kutasiriwa kinyume chake.

Hii ni dhana ambayo inapaswa kutekelezwa kwa kuzingatia akili na imani; kinyume kabisa cha utepetevu wa imani na maisha ya kiroho; misimamo mikali ya kiimani na kidini; kwani kwa makundi kama haya, uhuru wa kidini unaonekana kutishia mawazo na misimamo yao, mambo yanayohatarisha amani na utulivu duniani.

Askofu mkuu Dominique Mamberti anasema, Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walipokuwa wanakazia uhuru wa kidini si kwmaba, walikuwa wanaleta Mafundisho mapya ndani ya Kanisa, bali walipenda kupyaisha mang’amuzi ya wengi katika maisha ya binadamu yanayosaidiwa na akili na utashi; mambo msingi yanayomwajibisha binadamu katika utekelezaji wa maamuzi yake msingi.

Mwanadamu kisimngi anasukumwa kutafuta asili na ukweli mkamilifu, ambao ni Mwenyezi Mungu mwenyewe, kiini cha utendaji wa akili ya mwanadamu na chemchemi ya uhuru. Mwingiliano wa mambo yote haya unamwezesha mtu kutambua na hatimaye, kuthamini utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.








All the contents on this site are copyrighted ©.