2013-12-19 15:27:09

Waraka kuhusu Elimu Katoliki wazinduliwa mjini Vatican


Majiundo ya majadiliano ya kitamaduni katika shule za Kikatoliki: ili kuishi kwa pamoja utamaduni wa upendo. Ni hati iliyowasilishwa kwa waandishi wa habari mjini Vatican na Viongozi wakuu wa Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki, chini ya uongozi wa Kardinali Zenon Grocholewski

Ni hati ambayo imepitishwa na Baba Mtakatifu Francisko hapo tarehe 28 Oktoba 2013, kama kumbu kumbu ya miaka 48 tangu Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walipochapisha hati kuhusu elimu inayojulikana kama "Gravissimum Educationis". Hii ni hati muhimu sana kuwahi kutolewa baada ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Kardinali Grocholewski anasema, mwaka 2015, Kanisa litafanya Jubilee ya Miaka 50 tangu hati juu ya Elimu ilipochapishwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa vatican. Kanisa Katoliki limekuwa ni mdau mkubwa katika sekta ya elimu kwani kuna zaidi ya vijana billioni moja wanaopata elimu kutoka katika: shule na taasisi za elimu zinazosimamiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki. Kuna waalimu na wafanyakazi millioni 58 ambao wameajiriwa kwenye shule na taasisi hizi.

Takwimu zinaonesha kwamba, katika kipindi cha Mwaka 2008 hadi mwaka 2011 kumekuwepo na ongezeko kubwa la wanafunzi wanaosoma katika shule na taasisi za Kanisa Katoliki sehemu mbali mbali za dunia. Idadi hii imepungua Barani Ulaya, lakini imeongezeka Barani Afrika, Asia na Oceania. Idadi ya wanafunzi wanaosoma kwenye shule na taasisi za Kanisa katika nchi changa ingeweza kuongezeka, lakini kuna mambo kadhaa ambayo bado yanakwamisha jitihada hizi.

Baadhi ya sababu hizi ni vita, kinzani na majanga asilia. Kuna uhaba mkubwa wa waalimu duniani na kwamba, kuna upungufu wa waalimu millioni 1.7, ili kufikia lengo la kuwa na waalimu wenye sifa na ubora unaotakiwa na UNICEF. Hali hii ni mbaya zaidi Barani Afrika, kwani takwimu zinaonesha kwamba, kuna mwalimu mmoja kwa wanafunzi mia moja!

Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki limeendelea kusaidia kutoa utambulisho wa shule na taasisi zinazoendeshwa na kumilikiwa na Kanisa Katoliki. Kanisa linatambua kwamba, shule na taasisi hizi ni mahali pa ushuhuda wa imani unaowashirikisha, waamini walei pamoja na watawa ambao kwa kiasi kikubwa wanatekeleza utume wao kwenye sekta ya elimu.

Hati hii mpya anasema Kardinali Zenon Grocholewski inagusa kwa karibu zaidi changamoto mbali mbali za mwingiliano wa kitamaduni unaojitokeza kutokana na utandawazi na maendeleo sayansi na teknolojia. Walengwa wakuu wa hati hii ni wazazi na walezi we nye dhamana ya malezi na majiundo kwa watoto wao; waalimu, majaalimu na wafanyakazi ambao kwa pamoja wanaunda Jumuiya ya walezi.

Hati hii ni msaada mkubwa kwa Tume za Mabaraza ya Maaskofu kuhusu elimu pamoja na wadau mbali mbali wanaojihusisha na sekta ya elimu. Hii ni nyenzo ya majadiliano ya kitamaduni inataka kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu; uhuru wa kidini kwa kuzingatia utambulisho wa Kanisa Katoliki. Neno msingi ni majadiliano!

Lengo ni kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kitamaduni katika sekta ya elimu, ili kujenga na kuimarisha utamaduni wa upendo, dhamana inayotekelezwa na Kanisa katoliki katika sekta ya elimu na kama sehemu ya utangazaji wa Injili ya Furaha.

Askofu mkuu Angelo Vincenzo Zani, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la elimu anasema, tema ya majadiliano ni sehemu ya mchakato wa utume unaofanywa na Mama Kanisa katika sekta ya elimu. Hii ni changamoto iliyotolewa na Makardinali kunako Mwaka 2008 kwa kuhamasisha Kanisa kushirikiana na wadau mbali mbali katika sekta ya elimu, ili kuchangia maboresho ya elimu duniani. Kunako mwaka 2008, wawakilishi kutoka dini na madhehebu mbali mbali walichangia kuhusu umuhimu wa elimu katika mwingiliano wa tamaduni.

Baraza likaanza kazi yake kwa baraka na utashi wa Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI kunako mwaka 2011 muswada wa hati hii, ukapitishwa na wajumbe wa Baraza la Kipapa la elimu. Mang'amuzi ya majadiliano ya kitamaduni ni jambo ambalo limeonesha mafanikio makubwa sehemu mbali mbali za dunia.

Kunako Mwaka 2015 Kanisa litaadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican ulipochapisha Waraka kuhusu elimu. Mwaka huu pia Kanisa litaadhimisha Jubilee ya Miaka 25 tangu Katiba kuhusu elimu ilipochapishwa na kufanya rejea kuhusu vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu zinazomilikiwa na kusimamiwa na Kanisa Katoliki.







All the contents on this site are copyrighted ©.