Waraka kuhusu Elimu Katoliki wazinduliwa mjini Vatican
Majiundo ya majadiliano ya kitamaduni katika shule za Kikatoliki: ili kuishi kwa pamoja
utamaduni wa upendo. Ni hati iliyowasilishwa kwa waandishi wa habari mjini Vatican
na Viongozi wakuu wa Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki, chini ya uongozi wa Kardinali
Zenon Grocholewski
Ni hati ambayo imepitishwa na Baba Mtakatifu Francisko hapo
tarehe 28 Oktoba 2013, kama kumbu kumbu ya miaka 48 tangu Mababa wa Mtaguso mkuu wa
Pili wa Vatican walipochapisha hati kuhusu elimu inayojulikana kama "Gravissimum Educationis".
Hii ni hati muhimu sana kuwahi kutolewa baada ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.
Kardinali
Grocholewski anasema, mwaka 2015, Kanisa litafanya Jubilee ya Miaka 50 tangu hati
juu ya Elimu ilipochapishwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa vatican. Kanisa Katoliki
limekuwa ni mdau mkubwa katika sekta ya elimu kwani kuna zaidi ya vijana billioni
moja wanaopata elimu kutoka katika: shule na taasisi za elimu zinazosimamiwa na kuendeshwa
na Kanisa Katoliki. Kuna waalimu na wafanyakazi millioni 58 ambao wameajiriwa kwenye
shule na taasisi hizi.
Takwimu zinaonesha kwamba, katika kipindi cha Mwaka
2008 hadi mwaka 2011 kumekuwepo na ongezeko kubwa la wanafunzi wanaosoma katika shule
na taasisi za Kanisa Katoliki sehemu mbali mbali za dunia. Idadi hii imepungua Barani
Ulaya, lakini imeongezeka Barani Afrika, Asia na Oceania. Idadi ya wanafunzi wanaosoma
kwenye shule na taasisi za Kanisa katika nchi changa ingeweza kuongezeka, lakini kuna
mambo kadhaa ambayo bado yanakwamisha jitihada hizi.
Baadhi ya sababu hizi
ni vita, kinzani na majanga asilia. Kuna uhaba mkubwa wa waalimu duniani na kwamba,
kuna upungufu wa waalimu millioni 1.7, ili kufikia lengo la kuwa na waalimu wenye
sifa na ubora unaotakiwa na UNICEF. Hali hii ni mbaya zaidi Barani Afrika, kwani takwimu
zinaonesha kwamba, kuna mwalimu mmoja kwa wanafunzi mia moja!
Baraza la Kipapa
la Elimu Katoliki limeendelea kusaidia kutoa utambulisho wa shule na taasisi zinazoendeshwa
na kumilikiwa na Kanisa Katoliki. Kanisa linatambua kwamba, shule na taasisi hizi
ni mahali pa ushuhuda wa imani unaowashirikisha, waamini walei pamoja na watawa ambao
kwa kiasi kikubwa wanatekeleza utume wao kwenye sekta ya elimu.
Hati hii mpya
anasema Kardinali Zenon Grocholewski inagusa kwa karibu zaidi changamoto mbali mbali
za mwingiliano wa kitamaduni unaojitokeza kutokana na utandawazi na maendeleo sayansi
na teknolojia. Walengwa wakuu wa hati hii ni wazazi na walezi we nye dhamana ya malezi
na majiundo kwa watoto wao; waalimu, majaalimu na wafanyakazi ambao kwa pamoja wanaunda
Jumuiya ya walezi.
Hati hii ni msaada mkubwa kwa Tume za Mabaraza ya Maaskofu
kuhusu elimu pamoja na wadau mbali mbali wanaojihusisha na sekta ya elimu. Hii ni
nyenzo ya majadiliano ya kitamaduni inataka kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu;
uhuru wa kidini kwa kuzingatia utambulisho wa Kanisa Katoliki. Neno msingi ni majadiliano!
Lengo ni kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kitamaduni katika sekta ya
elimu, ili kujenga na kuimarisha utamaduni wa upendo, dhamana inayotekelezwa na Kanisa
katoliki katika sekta ya elimu na kama sehemu ya utangazaji wa Injili ya Furaha.
Askofu
mkuu Angelo Vincenzo Zani, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la elimu anasema, tema
ya majadiliano ni sehemu ya mchakato wa utume unaofanywa na Mama Kanisa katika sekta
ya elimu. Hii ni changamoto iliyotolewa na Makardinali kunako Mwaka 2008 kwa kuhamasisha
Kanisa kushirikiana na wadau mbali mbali katika sekta ya elimu, ili kuchangia maboresho
ya elimu duniani. Kunako mwaka 2008, wawakilishi kutoka dini na madhehebu mbali mbali
walichangia kuhusu umuhimu wa elimu katika mwingiliano wa tamaduni.
Baraza
likaanza kazi yake kwa baraka na utashi wa Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI kunako
mwaka 2011 muswada wa hati hii, ukapitishwa na wajumbe wa Baraza la Kipapa la elimu.
Mang'amuzi ya majadiliano ya kitamaduni ni jambo ambalo limeonesha mafanikio makubwa
sehemu mbali mbali za dunia.
Kunako Mwaka 2015 Kanisa litaadhimisha Jubilee
ya Miaka 50 tangu Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican ulipochapisha Waraka kuhusu elimu.
Mwaka huu pia Kanisa litaadhimisha Jubilee ya Miaka 25 tangu Katiba kuhusu elimu ilipochapishwa
na kufanya rejea kuhusu vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu zinazomilikiwa na kusimamiwa
na Kanisa Katoliki.