2013-12-19 11:07:18

Mwenyezi Mungu anaweza kumkirimia mwanadamu upya wa maisha hata katika Jangwa na Ugumba!


Unyenyekevu ni fadhila muhimu sana inayomwezesha Mwenyezi Mungu kushirikiana na binadamu katika kutekeleza mipango na malengo yake. Kwa njia ya unyenyekevu, Mwenyezi Mungu anaweza kufanya mambo ya ajabu hata pale ambapo mwanadamu alikwisha hesabika kuwa ni tasa na hawezi kuzaa tena.

Huruma na upendo wa Mungu unajionesha kwa namna ya pekee kwa wanawake tasa ambao kwa njia ya unyenyekevu wa maisha yao, Mwenyezi Mungu ameweza kuwainua kutoka mavumbini kama ilivyojionesha kwa Elizabeth, Mama yake Yohane Mbatizaji anayesimuliwa wakati huu wa Kipindi cha Majilio.

Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi, tarehe 19 Desemba 2013 kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican. Wanawake wagumba waliokuwa wamekata tamaa, wanaonja matumaini mapya kwa njia ya unyenyekevu mbele ya Mwenyezi Mungu.

Hii inaonesha kwamba, Mwenyezi Mungu ni muweza wa yote anaweza kuchipusha maisha mapya hata kwenye "Jangwa" la maisha ya mwanadamu na kwamba, Mwenyezi Mungu daima ni mwaminifu katika utekelezaji wa ahadi zake. Kwa njia ya ukombozi, anasema Baba Mtakatifu, Mwenyezi Mungu anamkirimia mwanadamu maisha, lakini jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, binadamu anashirikiana na Mungu katika utekelezaji wa mipango na mikakati yake.

Mwenyezi Mungu anampatia mwamini neema na baraka za kuweza kutembea katika hija ya utakatifu wa maisha. Huu ni mwaliko anasema Baba Mtakatifu kwa waamini kuomba neema na baraka hizi kwa kutambua mapungufu yao ya kibinadamu, ili waweze kuonja huruma na upendo wa Mungu, hata katika majanga ya maisha.

Waamini wanakumbushwa kwamba, kiburi ni chukizo mbele ya Mungu. Kipindi hiki cha Majilio, kiwawezeshe waamini kumtukuza, kumsifu na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema na baraka nyingi anazowakirimia katika maisha yao







All the contents on this site are copyrighted ©.