2013-12-18 08:16:32

Wasi wasi unazidi kuongezeka Afrika Magharibi kutokana na kinzani na migogoro ya kijamii


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Magharibi linalounganisha Maaskofu kutoka: Senegal, Mauritania, Cape Verde na Guinea Bissau, hivi karibuni limeonesha wasi wasi wake kutokana na kinzani, vurugu na vita inayoendelea katika baadhi ya nchi jirani. Maaskofu katika mkutano wao uliofanyika mjini Ziguinchor, Senegal, eneo lililotaka kujitenga na Senegal kunako mwaka 1982. RealAudioMP3

Maaskofu wamesali kwa ajili ya kuombea haki, amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa na kuzitaka Serikali zao, kuhakikisha kwamba, zinajenga mazingira yatakayowezesha wananchi kuishi kwa amani na utulivu. Maaskofu wanawaalika vijana kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu na kamwe wasitumiwe na baadhi ya wanasiasa wanaotaka kusababisha vita na machafuko kati ya watu.

Maaskofu wanasema wataendelea kushirikiana na viongozi wa kidini na wanasiasa wanaotaka kusimama kidete kulinda na kutetea mafao ya wengi na maendeleo ya wote. Ni mwaliko wa kukusanya nguvu za wananchi ili kulinda amani ambayo ni kielelezo na jina jipya la maendeleo endelevu.

Mkutano huu umehudhuriwa pia na Askofu mkuu Luis Mariano Montermayor, Balozi wa Vatican nchini Mauritania ambaye amekazia umuhimu wa majadiliano ya kidini na kiekumene kama nyenzo muhimu sana ya kudumisha misingi ya haki, amani na upatanisho. Wamekazia ujenzi wa umoja na mshikamano miongoni mwa vyuo vikuu vya Kikatoliki katika eneo hili.








All the contents on this site are copyrighted ©.