2013-12-18 07:52:35

Jifungeni kibwebwe kuwahudumia maskini mamboleo!


Ndani ya Kanisa waamini wanapaswa kujifunza kwamba Huduma ya Kiinjili haipaswi kumezwa na utukufu wala mafao ya mtu binafsi. Haya ni kati ya mafundisho makuu yanayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko na kujionesha kwa namna ya pekee katika ujumbe aliouandika kwa Padre Fray Josè Narlaly, Mkuu wa Shirika la Fumbo la Utatu Mtakatifu, linaloadhimisha Kumbu kumbu ya miaka 800 tangu alipofariki dunia Mtakatifu Juan de Mata na miaka 400 tangu alipofariki dunia Mtakatifu Yohane Batista wa Bikira Maria Mkingiwa dhambi ya asili, kiongozi aliyeleta mageuzi makubwa ndani ya Shirika hili.

Baba Mtakatifu anasema, watakatifu hawa hata kama walibahatika kwa namna ya pekee kuwa na maisha yenye heshima, utulivu na uhakika wa usalama, walipokea wito maalum kutoka kwa Mwenyezi Mungu, aliyewachangamotisha kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Baba Mtakatifu anasema, watakatifu hawa ni mfano bora wa kuigwa, kwani walikubali kupokea changamoto zilizojitokeza katika maisha yao na Kanisa linapowasherehekea wakati huu ni kwa sababu walijitosa kwa namna ya pekee, kupokea na kuubeba Msalaba wa Kristo katika hali ya unyenyekevu, wakajiachilia mikononi mwa Mungu bila kumwekea masharti wala vizingiti, ili aweze kutekeleza kazi miongoni mwa watu wake.

Kama ilivyokuwa kwa watakatifu hawa, waamini wote wanaalikwa kwa namna ya pekee kuonja ile furaha inayobubujika kwa kukutana na Yesu ili kuvuka vikwazo vya ubinafsi, raha na starehe, tayari kuwaendelea wote wanaohitaji kuona tena Mwanga wa Injili. Kwa miaka mingi Shirika la Fumbo la Utatu Mtakatifu, limekuwa ni maskani ya maskini; mahali ambapo watu waliojeruhiwa kiroho na kimwili wanagangwa kwa njia ya sala na huduma inayojikiza katika huruma na upendo.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, Shirika la Fumbo la Utatu Mtakatifu ni mfano bora wa kuigwa kwa kutambua kwamba, uongozi ndani ya Kanisa ni huduma, changamoto ya kujiondoa katika kishawishi cha mtu kujitafuta mwenyewe wala kugubikwa na uroho wa mali na madaraka.

Viongozi na waamini wajifunze kushirikishana karama na vipaji walivyopokea kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kwa kutambua kwamba, wanaalikwa kuwa ni wasimamizi bora na kwa ajili ya huduma kwa maskini ambao idadi yao inazidi kuongezeka siku hadi siku, kiasi kwamba, Kanisa haliwezi kuwafumbia macho kana kwamba, hawapo, bali wanapaswa kuonjeshwa huduma ya huruma na upendo.

Baba Mtakatifu anahitimisha ujumbe wake kwa Shirika la Fumbo la Utatu Mtakatifu kwa kuwasihi kumkumbuka katika sala na maombi yao katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, bila kuwasahau maskini, kwani wao kwa upande wao kamwe hawawezi kumsahau, kama alivyofanya Yesu Mwenyewe, kwa kuwapatia hifadhi katika sakafu ya moyo na utume wake hapa duniani; Yesu aliyetumwa na Baba yake wa mbinguni ili kuwatangazia maskini habari njema ya wokovu na kwa njia ya ufukara wake, akawakirimia wote utajiri usiokuwa na kipimo!







All the contents on this site are copyrighted ©.