2013-12-17 08:53:52

Kipindi cha Majilio na Noeli ni wakati wa mshikamano wa dhati na maskini!


Kanisa Katoliki nchini Ubelgiji linawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema katika kipindi cha Majilio na hatimaye Sherehe za Noeli, kujitahidi kumwilisha amri ya mapendo kwa Mungu na jirani, kwa kujitoa kimasomaso kuwasaidia watu wanaolazimika kuishi katika umaskini, ujinga na maradhi, ili nao pia waweze kuonja huruma na upendo wa Mungu kwa njia ya jirani zao. RealAudioMP3

Askofu Jean Kockerols, wa Jimbo Katoliki la Ypres, Ubelgiji katika barua yake ya kichungaji, anawaalika waamini pamoja na vyama vya kitume vinavyojitoa kwa ajili ya kuwasaidia maskini, kuendelea kufanya hivyo kwa ari na moyo mkuu kwani takwimu zinaonesha kwamba, idadi ya watu maskini hata nchini Ubelgiji katika kipindi cha Mwaka 2013 imeongezeka kwa asilimia 33.7%. Ongezeko hili ni sawa na asilimia 5.4% ya maskini nchini Ubelgiji kila mwaka. Hii ni hali ambayo kamwe haiwezi kukubalika kwani ni kielelezo makini cha ukosefu wa haki jamii.

Askofu Kockerols anasema, Noeli kiwe ni kipindi cha mshikamano wa upendo na udugu kati ya watu wa mataifa, ili kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kupambana na umaskini, ujinga na maradhi. Jamii ijifunze kugawana hata kile kidogo ilichonacho na wale ambao hawajabahatika kama wao!

Kwa njia hii, Noeli inaweza kusherehekewa na watu wengi zaidi na wala si kwa wale waliobahatika tu! Kuna idadi kubwa ya watu wanaoishi katika hali ya umaskini, watu ambao kwao baridi na hali ngumu ya maisha vimekuwa ni wimbo usiokuwa na kiitikio!








All the contents on this site are copyrighted ©.