2013-12-17 15:05:07

Jimbo kuu la Barcelona limempoteza Kardinali Ricardo Gordò


Kardinali Ricardo Maria Carles Gordò, Askofu mkuu mstaafu wa Jimbo kuu la Barcelona na Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania kuanzia Mwaka 1999 hadi mwaka 2005 amefariki dunia, Jumanne, tarehe 17 Desemba 2013 baada ya kuugua kwa muda mrefu. Mazishi yake yanatarajiwa kufanyika Jimbo kuu la Barcelona, Alhamisi, tarehe 19 Desemba, 2013.

Kardinali Ricardo Maria Carles Gordò alizaliwa tarehe 24 Septemba 1926. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, akapewa daraja Takatifu la Upadre hapo tarehe 29 Juni 1951. Baadaye akaendelea na masomo juu na kujipatia shahada za uzamivu katika Sheria za Kanisa kutoka katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Salamanca, kunako Mwaka 1953.

Tarehe 6 Juni 1969 akateuliwa na Papa Paulo VI kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki la Tortosa na hatimaye, akawekwa wakfu tarehe 3 Agosti 1969. Kama mchungaji mkuu wa Jimbo akajitosa bila ya kujibakiza kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Jimbo lake, kwa kuwashirikisha kwa namna ya pekee waamini walei ambao walichangia maendeleo na ustawi wa Kanisa, huku wakiyatakatifuza malimwengu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao.

Tarehe 23 Machi 1990, Papa Yohane Paulo II akamteuwa kuwa ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Barcelona. Akiwa anasukumwa na moyo wa kibaba na kichungaji akajenga utamaduni wa mabaraza ya Mapadre wa Jimbo pamoja na Mabaraza ya kichungaji ili kujipatia utambulisho wa Kikanisa, kwa kujenga na kuimarisha umoja, ili kwa pamoja waweze kutoka kifua mbele na kuzama katika mchakato wa Uinjilishaji.

Walengwa wakuu ni Waamini waliokuwa wamesahau mlango wa Kanisa kwa miaka kadhaa kutokana na sababu mbali mbali; wasioamini ili waweze kuonja Injli ya Furaha; vijana waweze kutumia karama na nguvu zao kumshuhudia Kristo; maskini, wahamiaji na familia. Alitafuta, akalea na kukuza miito mitakatifu; akaonesha kipaumbele cha pekee katika maisha na majiundo ya Mapadre wake tangu wakiwa Seminarini.

Alipenda kuona ushirikiano wa karibu na Maaskofu wake wasaidizi ambao walikuwa ni wanne, yote aliyafanya kwa sifa na utukufu wa Mungu. Alithamini sana utangazaji wa Injili kwa njia ya vyombo vya habari. Mwenyeheri Yohane Paulo II alimteuwa kuwa Kardinali tarehe 26 Novemba 1994.







All the contents on this site are copyrighted ©.