2013-12-17 10:11:04

Ibada zitakazoongozwa na Papa Francisko, Kipindi cha Noeli


Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuongoza Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican wakati wa kesha la Siku kuu ya Noeli kwa Mwaka 2013. Ibada hii itakayofanyika hapo tarehe 24 Desemba 2013, inatarajiwa kuanza saa 2: 45 za Usiku kwa Saa za Ulaya.

Jumatano tarehe 25 Desemba 2013, Siku kuu ya Noeli, yaani kuzaliwa kwa Yesu Kristo Mkombozi wa dunia, Baba Mtakatifu atatoa Ujumbe na Baraka za Noeli kwa Mji wa Roma na Ulimwengu katika ujumla wake, kama unavyojulikana kwa lugha ya Kilatini, "Urbi et Orbi" kuanzia saa 6:00 mchana kwa saa za Ulaya.

Jumanne tarehe 31 Desemba 2013, Kesha la Siku kuu ya Bikira Maria Mama wa Mungu na Siku ya 47 Kuombea Amani Duniani, Baba Mtakatifu ataongoza Masifu ya Jioni; Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu pamoja na Kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa shukrani kwa kuhitimisha Mwaka, kama unavyojulikana, "Te Deum".

Jumatano tarehe Mosi, Januari 2014, Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuongoza Ibada ya Misa Takatifu katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria Mama wa Mungu sanjari na Siku ya 47 ya Kuombea Amani Duniani, ambayo kwa Mwaka 2014 inaongozwa na kauli mbiu "Udugu ni msingi na njia ya amani". Ibada ya Misa Takatifu inatarajiwa kuanza saa 4:00 kwa saa za Ulaya.

Jumatatu tarehe 6 Januari 2014, Siku kuu ya Tokeo la Bwana au Epifania, Baba Mtakatifu Francisko kuanzia majira ya saa 4:00 asubuhi anatarajiwa kuongoza Ibada ya Misa Takatifu.

Taarifa hii imetolewa na Monsinyo Guido Marini mshereheshaji mkuu wa Ibada za Kipapa mjini Vatican, tarehe 17 Desemba 2013.







All the contents on this site are copyrighted ©.