2013-12-16 08:48:49

Katika mchakato wa ndoa na familia mhusisheni Mungu na Jamii, msiweke mkataba na shetani!


Tumsifu Yesu Kristo...!
Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican; katika kipindi kilichopita tulianza kuangazia juu ya maandalizi ya kupokea wito wa ndoa na kulijenga Kanisa la nyumbani. Tulikaza kusema, KWETU SISI TUNAOAMINI, NI MUHIMU KABISA TANGU MWANZO KUMHUSISHA MUNGU KATIKA MCHAKATO MZIMA NA KATIKA MAISHA YOTE YA NDOA [wapo wanaofanya makosa ya kumhusisha shetani tangu mwanzo; HAIFAI NI HATARI). Tulihimiza pia wanandoa WAJENGE UTUME WA KUOMBEANA KWA MUNGU NA KUPELEKANA KWA MUNGU. RealAudioMP3
Hili litarudiwa tena na tena! Ewe Mwanandoa ni mara ngapi unampigia Mungu goti kumwombea mwenzi wako? Bahati mbaya wengi huwa tunaombeana yanapotokea matatizo tu. Tukiwa katika heri, sala zinawekwa likizo. Ewe uliye katika ndoa, kuanzia leo punguza kelele, anza kusali kwa moyo kabisa kumwomba Mungu kwa ajili ya usitawi wenu na familia yenu.
Mlilie Mungu kwa machozi ya imani; hakika utauona wema wa Mungu. Mungu atakupa nguvu ya kuvumilia, na kwa uradhi wake, atakuondolea masumbufu hayo. Bwana alisema, ‘majaribu hayana budi kuja...,’ ndiyo maana twasema WANANDOA WAOMBEANE KWA MUNGU DAIMA, ili yule mwovu anayepanda mbegu ya chuki na fujo katika ndoa za watu ASIPATE NAFASI KAMWE. Mungu apewe nafasi ya juu kabisa. Leo tuendelee kwa kuangazia juu ya uhusika wa jamii katika maandalizi ya kuupokea wito wa ndoa na kulijenga Kanisa la nyumbani.
Mpendwa msikilizaji, kwa vile mwanadamu ni kiumbe jamii, maisha anayoyaishi yana athari pia katika jamii inayomzunguka. Ndoa ni wito na ni sakramenti ambayo ni muungano halali kati ya [mtu mume na mtu mke] mume mmoja na mke mmoja, nao wanafanywa kuwa mwili mmoja. Hawa wawili wanaofanya hesabu ya muungano, hawatoki hewani; wanatoka katika familia au jamaa inayowazunguka. Katika kuitikia wito wa ndoa, ni vema sana familia ikahusishwa tangu mwanzo. Familia isishitushwe tu kwamba kuna mtu ameongezeka, au mtu amehama ndani. Jamii isiadhibiwe kwa kushiriki tu katika matokeo mabaya ya miungano-holela.
Kushirikisha jamii ya karibu kadiri ya taratibu za jamii staarabu; kuna umuhimu wake. Jamii inaweza kuwa inamfahamu vizuri zaidi huyo unayependa kuwa naye kuliko unavyomfahamu wewe. Jamii pia inaweza KUKUSAIDIA KUMFAHAMU HUYO MCHUMBA WAKO NA ASILIA YAKE. Ni vema kabisa umfahamu vizuri huyo unayetaka kuingia naye katika agano ILI USIFANYE MAKOSA YA KUINGIA KATIKA AGANO NA MTU AMBAYE HUMFAHAMU.
Kwa msaada wa jamii yenye nia njema, unaweza kufanya maamuzi, yenye maana zaidi. Katika hili, tunawaonmba vijana wetu, SHIRIKISHENI WAZAZI MIPANGO YENU, LISHIRIKISHENI KANISA, MPATE BARAKA YA UCHUMBA.
Na wazazi nao kwa upande wao, waheshimu sana mielekeo sahihi ya watoto wao mintarafu wachumba; ili WAZAZI NA WALEZI WASIPITILIZE WAKAINGIA KATIKA KOSA LA KUWACHAGULIA WATOTO WAO WACHUMBA, kwa maslahi yao wazazi wenyewe. Matokeo yake vijana wataingia katika maisha ya ndoa kwa shinikizo-baridi la wazazi wao. Hapo tangu mwanzo furaha haipo katika ndoa za aina hiyo.
Wazazi na walezi, wasiwakatishe tamaa watoto wao, pale wanapowaletea habari za maelekeo ya kuupokea wito wa ndoa; lakini pia wasikubali harakaharaka na kuanza kupiga vigelegele kabla ya kuwasaidia vijana wao kuchunguza mazingira yote ya wachumba hao. Wazazi watoe miongozo, mafundisho na hata wazee wengine waalikwe watoe mang’amuzi yao namna ya kuhimili mikikimikiki mbalimbali ya maisha. Hapo kweli tutakuwa tunawasaidia vijana wetu. Lakini vijana nao wawe tayari kusaidiwa, kukuzwa.
Vijana wasomi wanaweza kukosea, wakadharau mang’amuzi ya wazee ambao hawakusoma. Kijana mpendwa, mwana wa Kanisa, zingatia neno hili: wazee wetu wana elimu ya mang’amuzi ambayo haijaandikwa katika vitabu vyovyote ulivyovisoma. UWE TAYARI KUULIZA, KUSIKILIZA, KUUTAFAKARI USHAURI WA WAZEE NA KISHA KWA BUSARA, KAMA YABIDI HIVYO, KUPOKEA.
Tunazidi kuomba hapa, vijana wetu wawe tayari kuendelea kukuzwa. WASIKUE KABLA YA UMRI. Familia na jamii ikikwepa jukumu la kuwasaidia na kuwaandaa vijana katika kuitikia wito wa ndoa na kujenga Kanisa la nyumbani; KAMWE HAITAKWEPA KUONJA MAUMIVU YA MADHARA YANAYOTOKEA katika miungano isiyo na misingi sahihi.
Tunamalizia kipindi hiki kwa kubainisha kwamba, maisha ya ndoa yenye mwanzo mwema, yatajenga Kanisa la Nyumbani lenye furaha na matumaini; na kwa lenyewe litakuwa zawadi na fahari kwa jamii inayowazunguka na tegemeo la Kanisa kwa ujumla. Tunawaweka mikononi mwa Mungu vijana wetu wote.
Mungu awajalie akili tambuzi ya kujua hadhi na uzito wa wito wa ndoa, awajalie utashi imara wa kuweza kuamua sawasawa na awajalie uradhi wa kuyakubali mapenzi yake katika kuitikia wito wa ndoa kwa ujasiri; ili MAISHA YA NDOA YASIWE KITU CHA KUDHARAULIWA BALI YAWE NI TUNU KWA WANADAMU, HESHIMA KWA MUNGU NA TUMAINI LA KANISA. Kutoka katika Studio za Radio Vatican, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.