2013-12-13 10:56:56

Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru wa Kenya


Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya, tarehe 12 Desemba 2013 amewaongoza wananchi wa Kenya kusherehekea Jubilee ya Miaka 50 tangu walipojipatia uhuru wa bendera kutoka kwa Mwingereza. Wananchi wamepongeza maendeleo makubwa yaliyokwisha kupatikana nchini Kenya na kusema kwamba, Kenya ingeweza kuwa imefika mbali kama rushwa, ufisadi, utawala mbaya na ukabila vingekuwa vimevaliwa njuga tangu awali!

Serikali ya Rais Uhuru Kenyatta kwa sasa inajielekeza katika mapambano dhidi ya umaskini, ujinga na maradhi; maadui watatu waliotambuliwa tangu Kenya ilipojipatia uhuru wake wa bendera miaka hamsini iliyopita chini ya Hayati Rais Jomo Kenyatta. Sherehe hizi zimehudhuriwa na wakuu wa nchi 14.

Mizinga 21 ilipigwa kama kielelezo cha shamrashamra hizi pamoja na gwaride la vikosi vya ulinzi na usalama kutoka Kenya vilivyoonesha ukakamavu mkubwa. Kenya inaendelea kucharuka katika uchumi, biashara na miundo mbinu. Jubilee ya miaka 50 ya Uhuru wa Kenya iwe ni fursa ya kufanya tafakari ya kina kuhusu: mafanikio, matatizo na changamoto zilizoko ili wananchi wa Kenya waweze kucharuka katika maendeleo yanayotoa kipaumbele cha kwanza kwa mafao ya wengi, binadamu na utu wake.

Rais Uhuru Kenyatta katika hotuba yake wakati wa Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru wa Kenya amesema, Serikali yake itaendelea kukazia ukweli na uwazi; inawahimiza wananchi kuchapa kazi kwa bidii, juhudi na maarifa na kamba, itawashughulikia bila huruma mafisadi na wote waliojipatia utajiri kwa njia isiyo halali na kwamba, kwa sasa kipaumbele cha kwanza ni utawala bora!







All the contents on this site are copyrighted ©.