2013-12-12 15:00:52

Papa- utu wa binadamu ni lazima kutetewa na kulindwa...


Baba Mtakatifu Alhamis hii majira ya asubuhi, aliwakaribisha na kuwahutubia, mabalozi waliowasilisha barua zao za utambulisho , kwa Jimbo Papa, tokea nchi zao. Mabalozi hao ni kutoka Algeria , Iceland, Denmark, Lesotho, Palestina, Sierra Leone , Cape Green , Burundi , Malta , Sweden , Pakistan, Zambia , Norway, Kuwait, Burkina Faso, Uganda na Yordan.

Katika hotuba yake, Papa aliwashukuru kwa salaam za matashi mema toka kwa viongozi wa nchi zao , na hivyo nae pia aliutumia muda huo kupeleka salaam zake kwa wakuu wa nchi hizo na pia kwa raia wote wa nchi zao.

Papa katika hotuba yake, alilenga zaidi matatizo na maovu yanayofanyika katika jamii ya nyakati hizi zetu, na hasa tatizo la watu kurubuniwa na kusafirishwa nje ya nchi zao kwa ahadi za uongo ambako heshima ya utu wao hudharirishwa na kutumikishwa nje ya ubinadamu. Na ametoa wito kwa jumuiya ya Kimataifa kuunganisha nguvu zake , kwa ajili ya kupambana na matatizo hayo.Papa ameonyesha imani yake kwamba, kwa juhudi za pamoja, madhulumu mengi dhidi ya haki za binadamu yanaweza kukomeshwa .
Kupitia Mabalozi hao,ameitaka jumuiya ya kimataifa kuongeza juhudi zake katika kutetea usawa, na kuwa na mkakati madhubuti wa kukomesha usafirishaji haramu wa watu, unaosikika kila sehemu ya dunia, hata katika nchi zenye viwanda vingi. Amekemea wanaume na wanawake, kutumiwa, kama chambo cha uchumi.

Adiha Papa pia ameonyesha kujali na kuitaka jumuiya ya kimataifa kuweka kipaumbele cha kwanza, katika mipango ya kufanikisha amani , mazungumzano na mahusiani mazuri kitamaduni, kisiasa , kiuchumi, na kujaribu kuyakoa maisha ya watu yanayo hatarishwa na matatizo mbalimbali.

Papa alieleza na kuonyesha kati ya masuala yanayomtia wasiwasi zaidi na ni ugandamizaji wa utu wa binadamu, kunakoonekana katika mfumo mpya wa usafirishwaji haramu wa watu, ambao ni aina mpya ya utumwa mambo leo , tatizo linalozidi kupanua makucha yake, ambalo lipo katika mataifa yote hata yaliyo endelea, na hugusa zaidi watu walio katika mazingira magumu kijamii: wanawake na wasichana , wavulana na wasichana , walemavu, maskini, ambao wengi wao ni kutoka familia maskini na wale wanao dharirishwa na migawanyiko ya kijamii .

Papa alisema, kwa Wakristo, huiona sura ya Yesu Kristo mteswa kwa watu hao wanaoteseka, wengi wao wakiteswa na umaskini na udhaifu wa kihali, akisema hata nje ya mtazamo wa imani ya kidini, kwa jina la ubinadamu wa kawaida, huonekana haja ya kushiriki kwa huruma, mateso ya watu hao wanyonge, kupitia utendaji wa hiari, wenye kujali mahangaiko yao.

Papa amesema kwa pamoja, ni lazima sote kuwa na jitihada za kuleta ukombozi dhidi ya mateso haya na hasa katika kukomesha biashara ya kutisha ya watu kusafirishwa na walaghai wachache wenye uchu wa fedha, wenye kuwaigiza mamilioni ya wahanga katika kazi ya kulazimishwa au kwa lengo la unyonyaji wa kinjisia na ngono.

Papa amekemea haya hayawezi kuendelea kuachwa hivihivi kama ilivyo, maana ni ukiukwaji wa haki za binadamu. Ni ukiukwaji wa utu wa mtu ,na ni kushindwa kwa jumuiya ya kimataifa.

Papa ameonyesha imani yake kwamba, jumuiya ya kimataifa, inao uwezo wa kukomesha hayo , iwapo itasimamia vyema uwepo wa usawa na mkakati madhubuti dhidi ya usafirishaji wa watu.

Na aliwaahidi Mabalozi kwamba, Jimbo la Papa liko tayari kutoa kila msaada unaoweza kuhitajika toka idara mbalimbali za Curia ya Roma, katika utendaji wa kazi zao. Na aliwatakia wingi wa baraka za Mwenyezi Mungu .









All the contents on this site are copyrighted ©.