2013-12-12 10:26:03

Heshima za mwisho kwa Tata Madiba!


Maelfu ya wanafamilia, viongozi wa serikali, viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa, watu mashuhuri, wageni na wananchi wa Afrika ya Kusini wanaendelea kutoa heshima zao za mwisho kwa mwili wa Marehemu Mzee Nelson Mandela aliyefariki dunia hapo tarehe 5 Desemba 2013 akiwa na umri wa miaka 95. Mwili wake umelazwa kwenye Jengo la Serikali, mjini Pretoria, mahali ambapo miaka 19 iliyopita aliapishwa kuwa Rais wa kwanza Mzalendo nchini Afrika ya Kusini.
Miaka 27 gerezani chini ya utawala wa Ubaguzi wa Rangi Afrika ya Kusini. Kunako Mwaka 1990 akawaomba wananchi wa Afrika ya Kusini kujikita katika haki, msamaha na upatanisho wa kitaifa. Mwaka 1994 akachaguliwa kuwaongoza wananchi wa Afrika ya Kusini, katika uchaguzi wa kwanza wa kidemokrasia nchini humo, utawala wa ubaguzi wa rangi ukatoweka!
Kwa siku ya Jumapili, macho ya wengi yataelekezwa Mashariki mwa Jimbo la Cape. Ndege ya kijeshi nchini humo itachukua mwili wa Mandela kutoka mji mkuu wa nchi hiyo, Pretoria hadi Mthatha, katika Jimbo la Mashariki ya Cape. Maelfu ya waombolezaji wanatarajiwa kujipanga kwenye mitaa kuanzia uwanja wa ndege wa mji huo, maarufu Mthatha kwa ajili ya kuangalia wanajeshi wanavyosafirisha mwili wa Mandela ukiwa kwenye jeneza kwenye gari la mizinga kuelekea kwenye kijiji cha Qunu, kilichopo Jimbo la Cape Mashariki ambako kiongozi huyo alilelewa tangu akiwa mtoto








All the contents on this site are copyrighted ©.