2013-12-11 07:36:41

Changamato katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya!


Mabadiliko ya sheria ya ndoa nchini Uingereza yanayotoa fursa sawa kwa ndoa za watu wa jinsia moja, mchango wa wahudumu wa maisha ya kiroho kwenye Hospitali na Magerezani ni kati ya maeneo ambayo yanaweza kuathirika sana kutokana na uamuzi wa Serikali ya Uingereza kuamua kubana matumizi. RealAudioMP3

Hizi ni kati ya changamoto zinazojitokeza katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, uliofungwa rasmi wakati wa Sherehe za Kristo Mfalme wa Ulimwengu.

Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza na Walles linasema, litaendeleza mchakato wa Uinjilishaji Mpya kama ilivyotangazwa na Mama Kanisa ili kukabiliana na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Haya ni kati ya mambo yaliyojiri wakati wa mkutano wa Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza uliohitimishwa hivi karibuni. Maaskofu wamejadili pia umuhimu wa Kanisa kuendelea kuwa makini ili kudhibiti vitendo vya nyanyaso za kijinsia dhidi ya watoto wadogo.

Askofu mkuu Antonio Mennin, Balozi wa Vatican nchini Uingereza ameshiriki pia katika mkutano huu. Maaskofu wamejadili kuhusu mashauri wanayopaswa kupewa Mapadre wanapohudumia ndoa za watu wa jinsia moja, zilizopitishwa nchini Uingereza na kwamba, sheria hii inatarajiwa kuanza kutumika Mwaka 2014. Kanisa Katoliki halitalazimika kisheria kufungisha ndoa za watu wa jinsia moja na kwamba, Mapadre na watawa wanaotoa huduma za maisha ya kiroho Hospitalini na Magerezani wataendelea na utume wao, kwani wao wanadhamana maalum katika maisha na ustawi wa wagonjwa na wafungwa: kiroho na kimwili.

Askofu mkuu Mennin amewasilisha salam na matashi mema kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko wakati wa mkutano wa Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza. Anawashukuru na kuwapongeza kwa mikakati makini ya shughuli za kichungaji wanayoitekeleza nchini Uingereza. Amewataka Maaskofu na waamini katika ujumla wao, kusimama kidete kulinda na kudumisha misingi ya ndoa na familia kadiri ya Mafundisho ya Kanisa, kwani ndoa za watu wa jinsia moja, zina athari kubwa katika maisha na ustawi wa familia.

Kanisa linakabiliana pia na changamoto za ufundishaji wa dini shuleni, ikiwa kama muswada wa sheria ya kifo laini utapitishwa nchini Uingereza na hivyo kuhalalisha mtu kuwa na haki ya kutema zawadi ya maisha. Askofu mkuu Mennin anawataka Maaskofu na waamini katika ujumla wao, kutokatishwa tamaa na changamoto hizi bali waendelee kusimamia kweli za Kiinjili, utu na maadili mema.

Amegusia vigezo vya kichungaji vilivyobainishwa na Baba Mtakatifu Francisko katika mchakato wa kuwatafuta Maaskofu watarajiwa, kwani hii ni dhamana nyeti na muhimu katika maisha na utume wa Kanisa.

Askofu mkuu Antonio Mennin anasema ataendelea kufanya hija za kichungaji kwenye Majimbo ya Kanisa Katoliki nchini Uingereza ili kufahamu: furaha, matumaini, kinzani, fursa na changamoto zinazojitokeza katika maisha na utume wa Kanisa nchini Uingereza.








All the contents on this site are copyrighted ©.