2013-12-10 12:06:06

Siku ya haki msingi za binadamu kimataifa: UN yamkumbuka Tata Madiba!


Jumuiya ya Kimataifa kila mwaka ifikapo tarehe 10 Desemba inaadhimisha Siku ya Haki msingi za binadamu na kwa namna ya pekee mwaka 2013, Umoja wa Mataifa unaadhimisha Miaka 20 tangu ulipofanyika mkutano wa haki msingi za binadamu, huko Vienna Austria na ukachangiwa na wadau mbali mbali na baadhi ya mafanikio yake yameanza kuonekana.

Katika kipindi cha miaka ishirini iliyopita, Umoja wa Mataifa umesimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu, kwa kukazia msingi wa sheria, kwa kuwasaidia waathirika pamoja na kuwahamasisha viongozi wa serikali kutekeleza wajibu wao msingi pamoja na kuvishirikisha vyama vya kiraia. Lengo ni kuwajengea watu uwezo wa kutambua na kusimamia haki zao msingi.

Ni sehemu ya ujumbe kutoka kwa Bwana Ban Ki-Moon, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, wakati wa Maadhimisho ya Siku ya haki msingi za binadamu, dhamana ambayo ni chanzo cha kuanzishwa kwa Umoja wa Mataifa, lakini utekelezaji wake, lazima ujioneshe katika utashi wa kisiasa kutoka kwa nchi wanachama. Haki msingi za binadamu zinapaswa kulindwa na kuendelezwa katika ngazi mbali mbali, ili kuzuia mauaji ya kimbari kama yalivyojitokeza katika baadhi ya nchi pamoja na uvunjifu mkubwa wa haki msingi za binadamu.

Umoja wa Mataifa kwa sasa umeanzisha kampeni inayopania kudhibiti vitendo vya uvunjifu wa haki msingi za binadamu; kwa kuzitambua na kuwajibika kuzilinda na kuzitetea. Jumuiya ya Kimataifa haina budi kutoa jibu la haraka katika maeneo ya uvunjifu wa haki msingi za binadamu. Nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa wanahamasisha kutekeleza ahadi zao kwa vitendo.

Siku hii, Umoja wa Mataifa unamkumbuka Mzee Nelson Mandela aliyesimama kidete kulinda na kutetea: utu na heshima ya binadamu, haki na amani. Ataendelea kukumbukwa kuwa ni kiongozi aliyetetea haki za binadamu kwa wote.







All the contents on this site are copyrighted ©.