Jumuiya ya Kimataifa inaomboleza Kifo cha Tata Madiba!
Viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa pamoja na wananchi wa Afrika ya Kusini wameanza kutoa
heshima zao za mwisho kwa Tata Madiba kwa sala kutoka kwa viongozi mbali mbali wa
kidini nchini Afrika ya Kusini. Mvua iliyokuwa inanyeesha imewazuia wananchi wa kawaida
kufika uwanjani ili kutoa heshima zao za mwisho kwa Mzee Nelson Mandela, lakini mvua
ni kielelezo cha baraka kwa makabila mengi Barani Afrika.
Katibu mkuu wa Umoja
wa Mataifa, Bwana Ban Ki-Moon katika salam zake za rambi rambi amesema, Afrika ya
Kusini imempoteza shujaa wake; imempoteza Baba na muasisi wa taifa la Afrika ya Kusini.
Jumuiya ya Kimataifa imempoteza kiongozi mashuhuri na mfano bora wa kuigwa katika
kutetea na kulinda haki msingi za binadamu.
Amepambana kufa na kupona kupinga
ubaguzi wa rangi, akawa ni mfano na kielelezo cha kiongozi anayetambua na kuthamini
msamaha. Amesimamia usawa, uhuru, haki, amani na demokrasia ya kweli.