2013-12-10 15:04:50

Guinea Bisssau Ijumaa kufunga na kusali kwa nia ya kuombea amani.


Askofu wa Jimbo Katoliki la Bissau, Askofu Jose Camnate na Askofu Pedro Zilli wa Jimbo Katoliki la Bafata katika nchi moja, wametoa mwaliko kwa waamini, Ijumaa 13 Desemba 2013, iwe ni Siku ya kufunga na kusali kwa ajili ya kuombea amani nchini mwao.

Taarifa iliyopelekwa katika vyombo vya habari Katoliki, imetoa ombi hilo la Maaskofu likiwataka Wakatoliki kusali zaidi kwa ajili ya kuombea amani na haki, wakisema ni Mungu tu anayeweza kuingilia kati, na kuleta utulivu wa kudumu katika taifa hilo.

Guinea-Bissau haijawahi kuwa na amani tangu kujipatia uhuru kutoka kwa Ukoloni wa Ureno mwaka 1974. Tangu wakati huo, kumekuwa na matukio mbalimbali ya serikali kupinduliwa na majaribio ya mapinduzi ya kijeshi. Maelfu ya watu waliuawa na mali kuharibiwa katika mapinduzi hayo. Ukosefu wa utulivu wa kisiasa uliosababishwa na jeshi, ni kati ya sababu kuu zinazo rudisha nyuma maendeleo ya taifa hilo hata leo hii.








All the contents on this site are copyrighted ©.