2013-12-09 08:29:19

Nia za jumla na kimissionari za Papa kwa mwezi Desemba 2013


Nia ya Baba Mtakatifu Francisko kwa mwezi Desemba ni ili kwamba, watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi waweze kupata hifadhi na kuonja upendo wa dhati. RealAudioMP3

Upendo ni kati ya mambo muhimu sana anayohitaji manadamu katika hija ya maisha yake hapa duniani, hata watoto wanahitaji kuonjeshwa upendo na mshikamano wa dhati, unaowawajibisha wadau mbali mbali, lakini kwa namna ya pekee dhamana hii nyeti inawagusa wazazi na walezi.

Kanisa linatambua umuhimu wa pekee walionao wazazi na walezi katika malezi na makuzi ya watoto wao, kwani familia ni mahali pa kwanza pa maisha ya kijamii na huduma; ni shule ya tunu msingi za kijamii na maendeleo yake. Ustawi na maendeleo ya watoto kwa kiasi kikubwa yanategemea sera na mikakati inayotolewa na Serikali husika, katika kuzijengea familia uwezo wa kutekeleza dhamana na majukumu yake kwa watoto mintarafu makuzi na malezi yao.

Kuna kilio kikubwa cha watoto kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaotafuta kuheshimiwa, kupendwa na kuthaminiwa; ili kulinda na kutetea haki zao msingi, utu na heshima yao, tangu pale wanapotungwa mimba, hadi mauti ya kawaida yanapowafika kadiri ya mpango wa Mungu, bila kuangalia hali ya mtoto kama ni mzima au ana ulemavu, wote ni zawadi kutoka kwa Mungu. Watoto hawa wameumbwa kwa sura na mfano wa mfano wa Mungu. Vitendo vyote vinavyokwenda kinyume na mwelekeo huu, havithamini haki msingi za watoto. Matendo adili yasaidie mchakato wa kulinda na kudumisha haki msingi za watoto sehemu mbali mbali za dunia.

Nia za kimissionari za Baba Mtakatifu Francisko kwa mwezi Desemba ni ili kwamba, Wakristo wakiangazwa na Neno wa Mungu aliyefanyika mwili, waweze kuwaandaa walimwengu kwa ajili ya ujio wa Mkombozi. Waamini wanaalikwa kwa namna ya pekee, kujiandaa kwa sala, tafakari ya Neno la Mungu na matendo mema kwa ajili ya ujio wa Yesu Kristo Masiha. Wahusika wakuu ambao ni Zakaria na Elizabeth, wachungaji wa kondeni, Mamajusi, watu wa kawaida lakini kwa namna ya pekee, Bikira Maria na Mtakatifu Yosefu wawe ni mfano bora wa kuigwa katika kipindi hiki cha Majilio! Hawa ni wale walioguswa kwa namna ya pekee na maandalizi ya ujio wa Masiaha.

Jambo la kujiuliza, Je, walimwengu wa nyakati hizi wanaonesha ari na mwamko wa kumngoja Masiha ili aweze kuzaliwa tena katika maisha yao? Pengine wanamwona kuwa ni kizingiti katika mikakati ya maisha yao? Mwelekeo huu upo pia kwa baadhi ya waamini wanaotaka njia ya mkato ili kufikia furaha. Licha ya mapungufu na majanga ya maisha, lakini bado watu wana kiu ya kutaka kukutana na Kristo, ili aweze kuleta magezi katika ulimwengu mamboleo. Haijalishi hata leo kusikia manabii wanaotangaza ukombozi wa chapu chapu lakini baadaye waamini wanajikuta wakichanganyikiwa na kukata tamaa ya maisha na hivyo hija ya Imani yao inaingiwa mchanga!

Yesu Kristo aliyezaliwa katika hali ya umaskini ni kielelezo kwamba, Yeye ndiye anayeweza kuzima kiu ya furaha na amani katika maisha ya mwanadamu. Kipindi cha Majilio, kiwe ni msaada kwa Waamini kujivika utu mpya kwa njia ya Sakramenti za Kanisa, Neno la Mungu na Matendo ya huruma kwa jirani. Waamini wajiandae kikamilifu wasijekujikuta Yesu anawafikia wakiwa bado wamemezwa na malimwengu. Waamini waandae mioyo na familia zao ili Kristo aweze kuzaliwa katika mazingira ya: Imani, Mapendo na Matumaini; Amani na mshikamano wa dhati kwa maskini na wote wanaosukimizwa pembezoni mwa Jamii: kiroho na kimwili.








All the contents on this site are copyrighted ©.