Serikali ya Kenya imetangaza kwamba, tarehe 13 Desemba 2013 itakuwa ni siku ya mapumziko
kitaifa, ili kuwapatia wananchi wa Kenya fursa ya kusherehekea Jubilee ya Miaka 50
tangu Kenya ilipojipatia uhuru wa bendera kutoka kwa Mwingereza. Taarifa zinaonesha
kwamba, maandalizi ya Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru wa Kenya yamekamilika.
Wananchi
wa Kenya wanaendelea kuhamasishwa ili kuhakikisha kwamba, Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru
wa Kenya, inakuwa ni fursa nyingine tena ya kujizatiti katika kuimarisha umoja na
mshikamano wa kitaifa; kukuza maendeleo ya kiuchumi kwa kuongeza: bidii, juhudi na
maarifa katika shughuli za uzalishaji na utoaji huduma.
Kilele cha Maadhimisho
ya Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru wa Kenya, ni Usiku wa manane hapo tarehe 12 Desemba
2013, Bendera ya Taifa itakapopandishwa kwa mara nyingine tena, kama ilivyofanyika
mwaka 1963.