2013-12-07 09:05:23

Ulimwengu wa digitali unakumbatia hali halisi ya maisha!


Kumtangaza Kristo katika nyakati hizi za dijitali ndiyo kauli mbiu iliyoongoza Maadhimisho ya ishirini na sita ya Mkutano mkuu wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Walei, ulioanza hapo tarehe 5 Desemba 2013 na kuhitimishwa rasmi tarehe 7 Desemba 2013 hapa mjini Vatican.

Wajumbe katika mkutano huu wameangalia kwa kina na mapana, maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari fursa na changamoto zake katika kufunga sehemu ya kwanza ya Karne ya ishirini na moja hasa katika matumizi ya mitandao ya kijamii, ambayo watumiaji wake wakuu kimsingi ni waamini walei.

Ni jukumu la Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, anaongeza juhudi, bidii na maarifa ya kuwatangazia Habari Njema ya Wokovu wale wanaoishi katika ulimwengu wa dijitali, ili waweze kuonja Injili ya Furaha inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Mitandao ya kijamii inatumika katika medani mbali mbali za maisha ya mwanadamu, kumbe Kanisa linapaswa kuifahamu vyema ili kuwafikia watumiaji wake.

Kardinali Stanislaw Rylko, Rais wa Baraza la Kipapa la Walei anasema kwamba, watumiaji wa mitandao ya kijamii wengi wao ni vijana. Mitandao ya kijamii iwasaidie vijana kugundua fursa zilizopo na athari zake, ili waweze kuwa makini, wasijekujikuta wanatumbukizwa kwenye "majanga ya maisha". Kanisa haliwezi kujiweka pembeni na kuwa mtazamaji wa matumizi ya mitandao ya kijamii, lazima lijiingize huko kwani, "utamu wa ngoma, ni kucheza" ndivyo wanavyosema Waswahili.

Professa Mario Pollo mmoja kati ya wawezeshaji wakati wa mkutano huu anasema kwamba, maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari yamemsaidia mwanadamu kupiga hatua kubwa ya maendeleo katika nyanja za mawasiliano ya kijamii, kiasi hata cha kubadili mfumo na mtndo wa maisha. Haya ni mawasiliano yanayosambaa kwa kasi ya ajabu, kiasi kwamba, muda si tatizo tena, kiasi kwamba zile Jamii ambazo zilizoea mawasiliano ya zawani zinajikuta zikichechemea ili kukabiliana na kasi na wingi wa habari unaotolewa.

Kwa upande wake, Professa Tonino Cantelmi amesema kwamba, maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari yamemwezesha mwanadamu kuwa na mwono mpya wa mahusiano yake na watu wengine. Amewataka wajumbe kutambua nguvu, fursa na athari zinazoweza kupatikana kutokana na maendeleo haya katika maisha ya mwanadamu. Watu wanapaswa kujifunza kuwa na matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii.

Professa Antonio Spadaro amewakumbusha wajumbe kwamba, ulimwengu wa digitali si wa kufikirika tu au unaoelea kwenye "Ombwe", bali ni sehemu ya ukweli wa maisha ya kila siku unaowagusa wengi, lakini kwa namna ya pekee vijana wa kizazi kipya. Kumbe, Mama Kanisa anawajibu wa kuwasaidia vijana kutambua fursa zinazoweza kupatikana kwenye mitandao ya kijamii sanjari na kung'amua athari zake, ili mitandao ya kijamii liwe ni Jukwaa jipya la Uinjilishaji kwa watu wanaoishi kwenye ulimwengu wa dijitali.

Huu ni ulimwengu unaokumbatia hali halisi ya maisha. Watumiaji wa mitandao wasijifungie tu huko, bali wanapaswa kutoka ili kujenga na kuimarisha mahusiano ya kijamii katika hali halisi ya maisha!







All the contents on this site are copyrighted ©.