Ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko kwa Siku ya 22 ya Wagonjwa Duniani kwa Mwaka 2014
Mama Kanisa kila mwaka ifikapo tarehe 11 Februari anaadhimisha Siku ya Wagonjwa Duniani
sanjari na Siku kuu ya Bikira Maria wa Lourdes. Mwaka 2014 Siku ya Wagonjwa Duniani
itaongozwa na kauli mbiu " Imani na Upendo: imetupasa na sisi kuutoa uhai wetu kwa
ajili ya hao ndugu" I Yoh. 3:16.
Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu Francisko
anapenda kutoa ujumbe huu kwa wagonjwa na wahudumu wa wagonjwa kutoka sehemu mbali
mbali za dunia, kutambua kwamba, wao ni kielelezo makini cha Kristo anayeteseka na
kwamba, wanabeba pamoja na Kristo mahangaiko yao ya ndani.
Kwa njia ya Fumbo
la Msalaba, Mwana wa Mungu amebomoa upweke wa mahangaiko na kutoa mwanga angavu, kielelezo
cha Fumbo la Upendo wa Mungu linaoimarishwa kwa njia ya mwanga wa Pasaka, tayari kuwa
na ujasiri wa kupambana na mahangaiko ya ndani kwa kutambua kwamba, Yesu yuko pamoja
nao katika mapambano haya!
Baba Mtakatifu anasema kwamba, kwa njia ya Fumbo
la Umwilisho, Mwenyezi Mungu hakuondoa hali ya magonjwa na mahangaiko katika maisha
ya mwanadamu, bali amejitwalia katika mwili wake, akayageuza na kuyapatia maana mpya
na maisha mapya, ili kwa kuungana na Kristo mateso na mahangaiko haya yaweze kupata
mwelekeo chanya.
Yesu ni njia na kwa nguvu za Roho Mtakatifu, waamini wanaweza
kupata ujasiri wa kumfuasa. Mwenyezi Mungu amemkirimia Mwanaye wa pekee pendo ambalo
amewamegea pia wanadamu, ili waweze kupendana wao kwa wao na kuthubutu kutolea maisha
yao kwa ajili ya jirani zao.
Baba Mtakatifu anasema, imani kwa Mwenyezi Mungu
mwingi wa huruma na mapendo inakuwa ni nguvu; imani kwa Yesu Kristo aliyeteswa inakuwa
pia ni nguvu ya kupenda hata adui. Mtihani wa imani kwa Kristo ni zawadi ya mtu kutolea
maisha yake kwa ajili ya jirani zake, hasa wale ambao ni maskini na wanyonge!
Kwa
njia ya sakramenti ya Ubatizo na Kipaimara, waamini wanaalikwa kujifananisha na Kristo,
Msamaria mwema kwa wote wanaoteseka na kusumbuka kwani katika hili, waamini wamelifahamu
pendo la Kristo, kwa kuwa Yeye aliutoa uhai wake kwa ajili yao, nao imewapasa kuutoa
uhai wao kwa jili ya hao ndugu.
Lengo ni kuwaonjesha wagonjwa matumaini na
tabasamu la Mungu kati ya Watu wake. Ukarimu unapaswa kuwa ni sehemu ya majitoleo
ya waamini kwa ajili ya watu wanaoteseka, kwa kuwaonjesha joto la upendo unaobubujika
kutoka katika Moyo Mtakatifu wa Yesu, ili kushiriki kikamilifu katimka ujenzi wa Ufalme
wa Mungu.
Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa siku ya ishirini
na mbili ya wagonjwa duniani kwa Mwaka 2014, anawalika waamini kukua na kukomaa katika
upendo unaoheshimu na kujali, kwa kuangalia na kuwakirimia wengine usalama wa maisha.
Bikira Maria alikuwa msikivu makini wa Neno la Mungu na mahitaji ya watoto wake.
Bikira
Maria kwa kusukumwa na huruma ya Kimungu ndani mwake, anajisahau na kutoka mbio kuelekea
Galilaya ili kukutana na binamu yake Elizabeth; alikuwa makini kusikiliza kilio cha
Wanaharusi wa Kana, walipotindikiwa na divai wakati wa sherehe; anabeba ndani mwake
katika hija ya maisha yake, maneno ya utabiri wa Mzee Simeoni kwamba, upanga utautoboa
moyo wake; kwa nguvu ya ajabu anadiriki kusimama chini ya Msalaba wa Yesu.
Baba
Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kumkimbilia Bikira Maria kwa imani, matumaini
na ibada kwa kutambua kwamba, atawasikiliza na kuwasaidia na kamwe hatawaacha! Bikira
Maria ni Mama wa Yesu Msulubiwa, aliyefufuka kutoka katika wafu: anayeendelea kuwa
pembeni mwa misalaba ya maisha ya wafuasi wake na kuwasindikiza katika hija ya ufufuko
na utimilifu wa maisha.
Baba Mtakatifu anasema kwamba, Mtakatifu Yohane alikuwa
na Bikira Maria chini ya Msalaba, anawasaidia waamini kutambua chemchemi ya imani
na mapendo yanayobubujika kutoka katika moyo wa Mungu ambaye ni Upendo. Anawakumbusha
waamini kwamba, hawawezi kumpenda Mungu bila kuwapenda jirani zao. Yeyote anayesimama
chini ya Msalaba pamoja na Bikira Maria anajifunza kupenda kama Yesu. Msalaba ni uhakika
wa upendo aminifu wa Mungu kwa ajili ya binadamu.
Ni upendo unaoingia katika
dhambi na kusamehe; unagusa mateso na mahangaiko ya binadamu na kuwakirimia nguvu
za kuweza kustahimili; anaingia katika kifo, ili kukishinda na kuokoa... Msalaba wa
Kristo unawaalika waamini kujiachilia ili waweze kuguswa na upendo wa Mungu; kuangalia
kwa huruma na mapendo, hasa wale wanaoteseka na wanaohitaji msaada.
Baba Mtakatifu
Francisko anahitimisha ujumbe wake kwa Siku ya 22 ya Wagonjwa Duniani kwa Mwaka 2014
chini ya maombezi ya Bikira Maria, ili awasaidie wagonjwa waweze kuishi mateso na
mahangaiko yao kwa kuungana na Yesu Kristo; awasaidie wale wanaowatunza wagonjwa kutekeleza
wajibu wao barabara. Baba Mtakatifu anatoa baraka zake za kitume kwa wagonjwa na wafanyakazi
wote katika sekta ya afya.
Ujumbe huu umetafsiriwa na Padre Richard A.
Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.