Mpendwa mwanatafakari wa neno la Mungu, kutoka katika Idhaa ya Kiswahili ya Radio
Vatican, tukiwa bado katika safari ya hija ya wokovu, maandalizi ya roho zetu kumpokea
Emanueli Mwana wa Mungu, Mama Kanisa haachi kutuwekea zawadi kichocheo cha imani na
furaha ya mioyo yetu. Zawadi hii ni fumbo la Kukingiwa Dhambi ya Asili Mama Bikira
Maria, Mama wa Mungu.
Mpendwa, wote
twajua kabisa kuwa kwa njia ya Adamu tumeingia duniani, na katika hali ya kawaida
twajua kuwa roho ikiungana na mwili lazima ipate madhara ya mwili na hivi kwa jambo
hili dhambi ya asili. Je inawezekanaje Mama huyu asipate dhambi hii? Swali hili limekuwa
likiulizwa tangu karne za kwanza za kanisa mpaka hivi leo. Mama Kanisa akisali sana
na kujikabidhi mbele ya Mungu akitazama Neno la Mungu na Mapokeo anaweka wazi ufunuo
wa Mungu mwenyewe akifundisha ulio ukweli wa ufunuo na kutangaza kuwa Bikira Maria
ni Imakulata.
Mama huyu anakingiwa dhambi ya asili kwa sababu lazima awe makao
stahili ya Mwana wa Mungu aliye mtakatifu, asiye na doa la dhambi. Ndiyo kusema kwa
vile Mwana wa Mungu ni mtakatifu asingeweza kuingia mahali pasipo patakatifu. Kumbe
kukingiwa dhambi ya asili kwa Mama Bikira Maria ni zawadi ya Kristo mwenyewe kwa mama
yake, na anaitoa zawadi hii mapema kwa mastahili ya msalaba atakaoupokea baadaye.
Mpendwa,
wazazi wetu wa kwanza walidanganywa na nyoka, wakaanguka katika dhambi ya kwanza,
wakapoteza utakatifu. Kukingiwa dhambi ya asili kwa Bikira Maria ni alama ya nguvu
ya Mungu juu ya dhambi iliyowaangusha wazazi hawa. Kumbe kwa fundisho hili la imani
tunaamini na kupata tumaini jipya kuwa kwa kuungana na Kristu dhambi na mwovu vitapatilizwa.
Mama
Kanisa anasherehekea sherehe hii kila tarehe 8 mwezi wa kumi na mbili kila mwaka.
Sherehe haitukuzi tu usafi na utakatifu wa Mama bali ni fundisho la imani ambalo twapaswa
kuliamini kina. Fundisho hili lilitangazwa na Baba Mtakatifu Pio IX mnamo tarehe 8Desemba
mwaka 1854 kuwa nguzo na fundisho sadikifu la imani.
Mama Kanisa anaposherehekea
sherehe hii anataka kila mmoja wetu akumbuke mwanzo wa ukombozi wetu. Mama huyu alikingiwa
dhambi ili aruhusu Mwana wa Mungu kutungwa mimba katika mji usio na doa na hivi nasi
katika utakatifu huo tunaweza kukombolewa. Kwa hakika hatuwezi kukombolewa na awaye
yote aliyeguswa na doa la dhambi bali tunakombolewa na asiyeguswa na doa la dhambi
naye ni Kristu Mwana wa Mungu.
Mama Bikira Maria alizaliwa kama ambavyo Mungu
alikuwa amekusudia mwanadamu awe tangu mwanzo. Fikiria juu ya Adamu na Eva kabla ya
kutenda dhambi yao ya kwanza, walikuwa watakatifu na wakaharibu utakatifu wao kwa
kiburi na tamaa ya ulimwengu. Kinyume nao Mama Maria anatunza utakatifu aliokabidhiwa
katika neema ya Mungu. Anakuwa tunda la kwanza la ukombozi. Anakuwa tabernakulo ya
kwanza kumbeba Mwana wa Mungu.
Mpendwa, kwa sherehe hii si tu tunakumbuka mwanzo
wa ukombozi wetu bali pia mwisho wa maisha yetu. Ndiyo kusema tunamwomba Mama atuombee
tuweze nasi kuonja matunda ya kazi ya mwanae, tuweze kuishi bila dhambi tukilenga
daima maisha ya utakatifu. Mama huyu ni mfano wa maisha bora, ni taa ambayo inaendelea
kuwaka anapojitokeza tena na tena katika maeneo mbalimbali akileta ujumbe wa mwanae
kwa mataifa. Ombi kwako mwana wa Mungu, ebu jaribu kufanya safari ya hija katika maeneo
mbalimbali ambayo mama kanisa ameyaratibisha ukaonje mapendo ya mama huyu.
Mpendwa
tukiendelea kusali kwa kujitayarisha kwa ajili ya majilio, tunawaombea wale wote waitwao
Imakulata wakashike vema utauwa wao, wakamwite Mama Maria Bikira akawaimarishe katika
utumishi wao kwa umma na kwa Kanisa. Tunawaombea Masista wote wanaotimiza miaka 25,
50 ya utawa, wanaoweka nadhiri za muda na za milele wakaimarishwe na Mama Bikira Maria
Msaada wa Daima. Tunaziombea Parokia zote na mashirika yote ya kitawa waliojiweka
chini ya ulinzi wa Mama Bikira Mkingiwa wa dhambi ya asili wakaimarike na kuwa safina
ya umoja, upendo na ustawi wa kiroho na hasa katika maisha ya sakramenti. Tumsifu
Yesu Kristu na Bikira Maria.
Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya,
C.PP.S.