2013-12-07 08:14:41

Nchi za Kiafrika kuendeleza ushirikiano wa karibu na Ufaransa


Ufaransa inaunga mkono juhudi zinazofanywa na nchi mbalimbali dhidi ya ujangili duniani kwani ujangili unaleta madhara makubwa kiuchumi, kiusalama na kimazingira. Rais wa Ufaransa Francois Hollande amesema hayo katika mkutano wa wakuu wa nchi za Afrika zinazokutana jijini Paris kujadili tishio la tembo na wanyama walio katika hatari ya kutoweka duniani.
Mkutano huo umefanyika tarehe 5 Desemba, jioni katika Hotel de la Marine, mjini Paris. Rais Jakaya Kikwete anahudhuria kikao hicho pamoja na viongozi wengine wakuu kutoka bara la Afrika. "Ufaransa iko tayari kushirikiana nanyi katika vita hii, tunahitajika kuchukua hatua dhidi ya ujangili na usafirishaji wa bidhaa zinazotokana na ujangili" amesema.
Amesema tafiti zinaonesha kuwa katika kipindi cha miaka 10 ijayo, kama kasi ya ujangili iliyoko sasa itaendelea, basi kuna hatari ya kupoteza moja ya tano ya tembo waliopo afrika na hasa Afrika ya Kati. "Ujangili ni tishio kubwa barani Afrika ni tishio kwa uchumi, tishio kwa usalama na pia kwa mazimgira, lazima tukomeshe ujangili na Ufaransa imeazimia kuchukua hatua"Amesema.
Amesema Ufaransa itaweka adhabu kali kwa makosa ya ujangili na kupiga marufuku biashara ya wanyama walio katika hatari na kwamba meno ya tembo yatakayokamatwa yataharibiwa kabisa. "Nataka ufaransa iwe mfano katika nchi za ulaya lakini na nchi za ki-Afrika lazma zichukue hatua kali na Ufaransa itashirikiana nanyi" Rais Hollande amesema.
Akichangia katika kikao cha viongozi wa Afrika, Rais Kikwete amezitaka nchi za kiafrika kujenga uwezo wa kupigana na ujangili na biashara ya tembo na kuzitaka nchi za kiafrika kuungana kuhakikisha biashara ya meno ya tembo inapigwa marufuku na masoko yake kufungwa. Mapema akihutubia katika kikao kuhusu uchumi baina ya Afrika -Ufaransa, Rais Kikwete amewaeleza wafanyabiashara wa Ufaransa kuwa bara la Afrika lina vigezo vyote vya kuwa na uchumi unaovuma duniani.
Amesema Afrika imejaliwa kuwa na maliasili nyingi kama ardhi, madini, mafuta, gesi, misitu na maliasili za baharini ambavyo vingi havijaendelezwa ipasavyo , na hii ina maanisha kuwa kuna nafasi nzuri barani humo. Amesema ili kufanikisha ukuaji huo "Afrika inahitaji ushirikiano na Ufaransa na nchi zingine kutoka nchi zinazoendelea na zilizoendelea kuzitumia maliasili hizi kwa ajili ya maendeleoā€¯.








All the contents on this site are copyrighted ©.