2013-12-07 11:55:23

Kampeni ya Kimataifa dhidi ya baa la njaa duniani!


Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linaunga mkono kampeni ya Shirikisho la Mashirika ya MIsaada ya Kanisa Katoliki Kimataifa, Caritas Internationalis katika mapambano dhidi ya baa la njaa duniani.

Kilele cha kampeni hii ni hapo tarehe 10 Desemba, 2013, Siku ya Kimataifa ya Haki Msingi za Binadamu. Baraza la Maaskofu Katoliki Canada kwa takribani miaka 45 limekuwa mstari wa mbele katika mchakato wa kusaidia maendeleo endelevu katika nchi changa zaidi duniani, kwa kushirikiana na Caritas Internationalis.

Lengo ni kuendelea kuhimiza wakuu wa Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba wanachukua hatua madhubuti na sera makini zitakazosaidia kupambana na baa la njaa duniani; kwa kuheshimu haki ya mtu kupata chakula bora na hasa zaidi chakula kinachozalishwa katika maeneo yake.

Mshikamano wa sala utafanyika kwenye Parokia na shule na taasisi mbali mbali zinazoendeshwa na kumilikiwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Canada. Mshikamano huu unaoneshwa pia na waamini katika sehemu nyingine za dunia. Ni matumaini ya Caritas Internationalis kwamba, kwa njia ya ushirikiano wa kimataifa unaozingatia kanuni auni, inawezekana kwa Jumuiya ya Kimataifa kutokomeza baa la njaa na utapiamlo ifikapo mwaka 2025.

Jumuiya ya Kimataifa haina budi kuhakikisha kwamba, kila mtu anahishi maisha yenye hadhi, bila kusumbuliwa na baa la njaa na utapiamlo; wala wasiwasi wa ukosefu wa uhakika wa usalama wa chakula wala watoto kukumbwa na utapiamlo wa kutisha unaohatarisha makuzi na maisha yao kwa sasa na kwa siku za usoni!







All the contents on this site are copyrighted ©.