2013-12-07 07:38:13

Changamoto za Uinjilishaji mpya nchini Ghana


Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana hivi karibuni limehitimisha mkutano wake mkuu wa Mwaka kwa kuwashukuru watu wa Mungu nchini humo kwa kufanikisha uchaguzi mkuu kwa amani na utulivu. Uinjilishaji mpya kama njia ya kutangaza imani ya Kikristo nchini Ghana ndiyo kauli mbiu iliyoongoza mkutano wa Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana. RealAudioMP3

Hata baada ya kusherehekea miaka 500 ya Ukristo nchini Ghana, Mama Kanisa bado anaona haja ya kuzamisha mizizi ya imani katika maisha na vipaumbele vya wananchi wa Ghana. Uinjilishaji mpya kama lengo la jumla, unapania kumwezesha mwanadamu kukutana na Mwenyezi Mungu, chemchemi ya uzima na amani kwa njia ya yesu Kristo. Mwenyezi Mungu anapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza, utu na heshima ya mwanadamu vikiheshimiwa na kuthaminiwa. Waamini wanaalikwa kuishuhudia imani yao kwa Kristo na Kanisa lake kwa njia ya vitendo.

Maaskofu wanasema, Ghana watu wana mwamko wa imani, amani na demokrasia na kwamba, kuna ushiriki mkubwa katika maisha ya kidini hali inayojionesha hata miongoni mwa wanasiasa. Pamoja na cheche hizi za mafanikio, baadhi ya watu wanaanzaa kupata ukakasi na ubaridi wa Injili, kiasi cha kutojisikia tena kwamba, wanachangamotishwa kujitosa kimasomaso kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake. Wakristo kila jumapili wanajaza Makanisa, lakini bado hawajaonesha ushuhuda wenye mvuto na mashiko katika maisha yao ya hadhara wanasema Maaskofu.

Uinjilishaji mpya hauna budi kugusa roho ya mtu, ili aweze kutubu na kumwongokea Mungu, huku akikumbatia utakatifu wa maisha. Hii ni changamoto endelevu kwa Familia yote ya Mungu nchini Ghana. Maaskofu wanasema, kuna mila, tamaduni na desturi njema; maisha adili; upendo kwa Mungu na jirani; ukarimu kwa jirani; dhana ya kupenda na kuheshimu uhai; mambo yote haya ni msingi thabiti wa imani unaoweza kusaidia mchakato wa waamini nchini Ghana kuwa kweli ni chumvi na mwanga wa mataifa.

Maaskofu wanasema, Familia ni kati ya taasisi zinazohitaji kuinjilishwa kwani inakumbana na changamoto nyingi za maisha, ili iweze kutekeleza wajibu na majukumu yake kadiri ya mpango wa Mungu kwa mwanadamu. Tunu msingi za maisha ya ndoa na familia hazina budi kulindwa na kutetewa na Serikali na kwamba, hili ni jukwaa makini la Uinjilishaji. Dhamana hii inaweza kutekelezwa kwa kuvihusisha vyama vya kitume kwa ajili ya familia. Wazazi na walezi watekeleze dhamana yao kwa uaminifu na uadilifu, kwa kutambua kwamba, wao ni vyombo vya kwanza kwa urithishaji wa tunu msingi za maisha ya kiutu, kimaadili na kiimani. Wawe ni ya chachu uchaji wa Mungu, ukweli, uaminifu na wachapa kazi; tunu zinazopaswa kujionesha tangu katika maisha ya kifamilia.

Maaskofu wanawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema nchini Ghana kusimama kidete kulinda na kutetea misingi ya haki, amani na utulivu; waendelee kuwa ni wadau na watetezi wa mazingira. Wapinge rushwa na ufisadi kwa matendo, wasimamie haki na mafao ya wengi pamoja na kutunza ardhi kwa ajili ya kizazi cha sasa na kile kijacho! Wanasiasa watekeleze wito na wajibu wao kwa kuongozwa na tunu msingi za Kiinjili, daima wakijitahidi kuwa kweli ni mfano wa kuigwa.

Maaskofu wanakazia Uinjilishaji unaokwenda sanjari na katekesi ya kina. Biblia, Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki na Mkusanyiko wa Mafundisho Jamii ya Kanisa na Nyaraka za Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican ni nyenzo muhimu sana katika azma ya Uinjilishaji kwa watu wa kizazi kipya. Waamini na watu wenye mapenzi mema, waendelee kuchota utajiri kutoka katika nyaraka hizi sanjari na kujikita katika mchakato wa utamadunisho.

Wananchi wa Ghana wasimezwe na malimwengu kwa kupenda sana mali na madaraka, mambo yanayopelekea rushwa na ufisadi wa mali ya umma. Rushwa imeenea katika medani mbali mbali za maisha ya wananchi wa Ghana! Watu wakatae kutoa na kupokea rushwa kwani ni kinyume cha haki msingi za binadamu. Maaskofu wanahimiza Serikali na vyombo husika kuhakikisha kwamba, vinatekeleza wajibu wake barabara!

Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana linakemea vikali ukabila na udini unaohatarisha umoja na mshikamano wa kitaifa na wanasema kwamba, tofauti hizi ni kielelezo cha utajiri wa wananchi wa Ghana na kamwe yasiwe ni mambo yanayowaga na kuwasambaratisha wananchi wa Ghana. Mwishoni, Maaskofu wanawaalika waamini kujenga na kuimarisha ari na moyo wa sala, kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya.








All the contents on this site are copyrighted ©.