2013-12-05 08:01:40

Miaka 50 ya Intermirifica: mwaliko wa kusikiliza, kujadiliana na kuwasiliana, ili Kristo afahamike na kupendwa na wengi!


Mama Kanisa anaadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican ulipochapisha waraka kuhusu njia za mawasiliano ya Jamii kwa Kilatini, Intermirifica. Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii, anawaalika waamini na watu wenye mapenzi mema kujenga na kudumisha utamaduni wa kusikiliza na kujadiliana ili kumpeleka Kristo kwa watu wote wanaokutana nao katika hija ya maisha yao hapa duniani.

Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii katika Maadhimisho haya, limezindua Mtandao wake mpya wa mawasiliano unaoweza kutembelewa kwa anuani ifuatayo: www.intermirifica50.va. Kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii wanaweza kupata ujumbe huu kwa njia ya twitter kwa anuani ifuatayo: @pccs.va.

Wakati huo huo, Chuo Kikuu cha Kipapa cha Laterano kimeadhimisha Jubilee ya Miaka 50 ya Waraka wa Intermirifica kwa Kongamano la kimataifa, kuhusu umuhimu wa njia za mawasiliano katika maisha na utume wa Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.