2013-12-04 09:07:16

Papa Francisko kutembelea Hospitali ya Bambino Gesù ili kusalimiana na watoto wagonjwa hapo tarehe 21 Desemba 2013


Askofu mkuu Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, amewashukuru wanamuziki na wageni mbali mbali walioshiriki katika tamasha la muziki kwa ajili ya kuchangia gharama za ukarabati na ununuzi wa vifaa vya kisasa kwa ajili ya Hospitali ya Bambino Gesù inayomilikiwa na kuendeshwa na Vatican. Hospitali hii ni kielelezo cha mshikamano wa dhati unaoneshwa na Mama Kanisa kwa watoto wagonjwa kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Askofu mkuu Parolin anasema, watu wenye karama na vipaji kutoka medani mbali mbali za maisha wanaweza kushirikiana na kushikamana kwa ajili ya kuwaonjesha wengine huruma na upendo, kwa njia ya kuwajengea madaktari na wauguzi uwezo na nyenzo zinazowawezesha kutoa huduma makini na za kisasa kwa watoto wagonjwa. Hospitali ya Bambino Gesù haina budi kuonesha mazingira ya ukarimu na huruma kwa watoto wagonjwa pamoja na wazazi na walezi wanaowahudumia wanapokuwa Hospitalini hapo.

Kutokana na kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya watoto wagonjwa, Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa Jumamosi, tarehe 21 Desemba 2013 kuwatembelea watoto wagonjwa waliolazwa kwenye Hospitali ya Bambino Gesù iliyoko mjini Roma. Jamii bora inapimwa kwa huduma makini inayotolewa kwa wanyonge na wagonjwa.

Hija hii ya kichungaji kama ilivyokuwa kwa watangulizi wake, Baba Mtakatifu Francisko anapenda kuwaonjesha watoto wagonjwa huruma na upendo unaobubujika kutoka kwa Mama Kanisa, kama sehemu ya mchakato unaopania kuwajengea watoto hawa matumaini ya leo na kesho iliyo bora zaidi. Wadau mbali mbali wanaendelea kuhimizwa kuboresha huduma kwa watoto wagonjwa kwani huu ni utume unaobubujika kutoka katika Injili ya Furaha.







All the contents on this site are copyrighted ©.