2013-12-03 07:48:39

Ujumbe wa amani na matumaini kwa wananchi wa Sudan ya Kusini


Maadhimisho ya Mwaka wa Imani imekuwa ni nafasi kwa waamini kujikumbusha kwamba, wanaitwa na kutumwa kila siku na Yesu Kristo ili kutangaza Injili ya furaha hadi miisho ya dunia kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao. Maaskofu wakiwa wameungana na Baba Mtakatifu wanahimizwa kuwaimarisha ndugu zao katika misingi ya imani, maadili na utu wema, daima wakipania kujenga umoja na mshikamano thabiti ndani ya Kanisa na kati ya watu wa mataifa. RealAudioMP3
Hii ni sehemu ya ujumbe wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kusini mwa Sudan, mara baada ya kufunga Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Wanasema, Kanisa linaadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu Papa Yohane wa XXIII alipochapisha Waraka wa Kichungaji, Amani Duniani, Pacem In Terris, kwa ajili ya Watu wote wenye mapenzi mema. Ni waraka unaokazia: haki na amani inayopatikana kwanjia ya majadiliano ya ushirikiano kati ya watu; amani kama kikolezo cha maendeleo; hati na dhamana ya watu ndani ya Jamii sanjari na mafao ya wengi.
Waraka huu unabubujika utajiri wa Kiinjili unaofumbata tunu msingi za kiutu zinazohifadhiwa kwenye sakafu ya mioyo ya binadamu. Ni Waraka unaoonesha sauti ya kinabiii inayotolewa na Mama Kanisa kwa watu wa nyakati hizi, mwaliko wa kutubu na kumwongokea Mungu, ili kuweza kuwa kweli ni watu wapya ndani ya Kristo.
Maaskofu wanaendelea kusema kwamba, wananchi wa Sudan ya Kusini wanfurahia sasa demokrasia na amani; wanaendelea kujenga na kuimarisha moyo wa majadiliano ya kidini na kiekumene kwa kushirikiana katika kutafuta mafao ya wengi nchini Sudan ya Kusini. Hata pale wanaposigana bado kuna matumaini na mwelekeo chanya wa kuweza kupata suluhu ya kudumu.
Maaskofu Katoliki Sudan ya Kusini wanasikitika kusema kwamba, rushwa, upendeleo na ukabila ni kati ya mambo yanayosababisha kero. Kuna haja ya kuimarisha misingi ya ukweli na uwazi, huduma na mafao ya wengi pamoja na kubainisha vipaumbele vichache vinavyoweza kutekelezeka kwa ajili ya maendeleo ya watu.
Wananchi wajitahidi kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa, kinzani na migogoro inayojitokeza miongoni wa mwa wananchi wa Jonglei ni jambo lisilokubalika kamwe, kwani Sudan ya Kusini inajengwa na watu kutoka katika kila kabila, lugha na jamaa. Wananchi wa Jonglei wanahimizwa kusimama kidete kulinda na kutetea misingi ya amani na kwamba, Kanisa liko pamoja nao!
Maaskofu wanasema kuwa uhusiano kati ya Sudan Kongwe na Sudan ya Kusini si mzuri sana, kumbe, kuna haja ya kuendeleza jitihada za makusudi ili kujenga na kuimarisha uhusiano katika nyanja mbali mbali za maisha kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Sudan katika ujumla wake. Wananchi wanaorudi Sudan ya Kusini baada ya vita na kinzani za kijamii, waonjeshwe ukarimu na upendo, ili waweze kuanza tena maisha mapya.
Maaskofu Kusini mwa Sudan wanasema, tatizo la Jeshi la Waasi kutoka Uganda pamoja na suala la Abyei ni mambo nyeti yanayopaswa kushughulikiwa kikamilifu ili: haki, amani, utulivu na maendeleo ya kweli yaweze kupatikana. Mchakato huu uwe ni sehemu ya mikakati ya uponyaji na upatanisho nchini Sudan ya Kusini; mchakato ambao unawahusisha wadau mbali mbali nchini Sudan. Maaskofu wanaipongeza Tume ya Kitaifa ya Uponyaji, Amani na Upatanisho na kwamba, wataendelea kuunga mkono juhudi hizi kwa kupitia Tume ya Haki na Amani.








All the contents on this site are copyrighted ©.