Simameni kidete kulinda na kutetea familia kwani ni kwa ajili ya mafao ya wengi!
Shirikisho la maisha ya Familia Barani Afrika, lililowakutanisha wajumbe kutoka katika
vyama vya kitume 28 vinavyowakilisha nchi 22 , limehitimisha kongamano lake la tatu
kimataifa chini ya usimamizi wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika
na Madagascar, SECAM na kuhudhuriwa na Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa
linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki Cor Unum. Mkutano huu ambao umefanyika nchini
Mauritius kwa kuongozwa na kauli mbiu “Familia kama mafao ya wengi; tusimame kidete
kuilinda”.
Shirikisho
hili linapata chimbuko lake katika Mafundisho ya Mababa wa Kanisa kwa kutambua kwamba,
familia ni msingi wa maisha ya binadamu, jamii na Kanisa katika ujumla wake na kwamba,
maendeleo na ustawi wa jamii kwa siku za usoni unategemea kwa kiasi kikubwa familia.
Katika kongamano la siku tatu, wajumbe pamoja na mambo mengine waliangalia:
vitisho dhidi ya utu na heshima ya binadamu; utekelezaji wa mikakati ya Cairo kuhusu
sera za maendeleo kwa Mwaka 2013 na baadaye mintarafu Bara la Afrika. Mikakati ya
kulinda na kutetea tunu msingi za maisha ya kifamilia dhidi ya utandawazi; familia
na majiundo ya mtu; mahusiano kati ya mwanaume na mwanamke; umuhimu wa kutunza usafi
wa moyo; changamoto za useja katika maisha ya kifamilia; huduma ya maisha katika utume
wa familia.
Wajumbe wamevipongeza vyama vya kitume kwa ajili ya familia vinavyojitoa
bila ya kujibakiza kwa ajili ya majiundo makini ya vijana wa kizazi kipya katika mchakato
wa kupambana na mmong’onyoko wa maadili na utu wema pamoja na maambukizi mapya ya
ugonjwa wa Ukimwi, bila kusahau maandalizi kabla ya ndoa.
Wanandoa wanapenda
kutoa changamoto kwa SECAM kuhakikisha kwamba, inasaidia kwa hali na mali majiundo
ya wahudumu wa maisha ya ndoa na familia, ili kusaidia kuimarisha tunu msingi za maisha
ya ndoa na familia kadiri ya mapenzi ya Mungu, mafao ya familia kwa kukumbatia Injili
ya Uhai. Familia ni mahali panapoonesha ukarimu wa kuwapokea na kuwalea watoto; ni
jukwaa makini la malezi kwa watoto na mahali pa kurithisha tunu bora za maisha. Hii
ni kanuni msingi kwa wana chama wa Shirikisho hili.
Washiriki wa kongamano
hili wanalipongeza Kanisa kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utamaduni wa maisha
na familia na kwamba, kama Waafrika, wanathamini sheria asilia za maumbile, maisha
ya binadamu, jumuiya na familia na kwamba, wanathamini mila na desturi njema zisizosigana
na Injili. Wanaitaka Familia ya Mungu Barani Afrika kuwa makini dhidi ya vitisho vinavyojitokeza
katika maisha ya ndoa na familia.
Athari za myumbo wa uchumi kimataifa ni
kati ya mambo yanayotaka kupelekea baadhi ya Jamii za Kiafrika kukengeuka kwa kuacha
misingi ya maadili na utu wema kama njia ya kupata fedha na misaada, jambo ambalo
kamwe haliwezi kukubalika! Watu wasimame kidete kutetea na kulinda familia dhidi ya
sera dhidi ya ongezeko la watu zilizopitishwa kwenye mkutano wa idadi ya watu kimataifa,
uliofanyika mjini Cairo kunako Mwaka 1994 sanjari na Itifaki ya Maputo.
Wajumbe
wa Kongamano la Shirikisho la Maisha ya Familia Barani Afrika wanasema, wanapenda
kusimama kidete kumwilisha kwa umakini mkubwa mafundisho ya Kanisa kuhusu ndoa na
familia na kamwe, watu wasikubali kukengeuka dhidi ya tunu msingi za maisha, utu na
heshima ya binadamu, kwani familia kadiri ya mapokeo, mila na tamaduni nyingi za Kiafrika
ni madhabahu ya upendo, maisha na tumaini la mwanadamu kwa siku za usoni.
Wajumbe
wanaipongeza SECAM kwa sera na mikakati ya kichungaji kwa ajili ya familia Barani
Afrika. Wanaomba Mabaraza ya maaskofu mahalia kuhakikisha kwamba, Makleri wanapata
majiundo makini kwa ajili ya ndoa na familia wanapokuwa kwenye malezi; Kanisa liendelee
kushirikiana na wanasiasa wanaotetea na kusimamia tunu msingi za maisha ya ndoa na
familia na thamani ya maisha katika maeneo yao na kamwe wasichoke kulinda na kuitetea
familia.
Imeandaliwa na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican.