2013-12-03 09:07:22

Mwaka wa Uinjilishaji Mpya unapania kuwaonjesha watu Injili ya Furaha kwa kukutana na Kristo!


Maadhimisho ya Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio, Jimbo kuu la Castries nchini Antille ni mwanzo wa Mwaka wa Uinjilishaji Mpya unaopania kuchochea mwamko wa utangazaji wa Injili ya Furaha miongoni mwa wananchi wa Saint Lucia.

Ni mwaliko kwa waamini kuwaonjesha jirani zao huruma na upendo wa Mungu uliofunuliwa kwa njia ya ujio wa Yesu Kristo Masiha na Mkombozi wa dunia. Ni mwaliko wa kuimarisha imani kwa Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai na kwamba, wote wanakaribishwa kushiriki katika karamu ya upendo inayoandaliwa na Kristo mwenyewe.

Kanisa kwa asili ni la Kimissionari, utume ambao unabubujika kutoka katika Fumbo la Utatu Mtakatifu, changamoto ya kuimarisha umoja na mshimano wa Kikanisa na kwamba, kila mwamini anachangamotishwa na Mama Kanisa kushiriki kwa ukamilifu katika dhamana hii, hasa katika ulimwengu wa utandawazi, unaotaka kumng'oa Mungu katika maisha na vipaumbele vya mwanadamu.

Ni mahubiri yaliyotolewa na Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu wakati wa hija yake ya kichungaji nchini Antilles, iliyoko kwenye Visiwa vya Caribbean sanjari na uzinduzi wa Mwaka wa Uinjilishaji Mpya, unaowasukuma waamini kutolea ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake; wakiwamegea wengine Injili ya Furaha inaojikita katika huruma na upendo wa Mungu kwa waja wake.

Waamini waitambue imani yao na kujitahidi kuwashirikisha wengine kwa kuwaendea hasa wale walioko pembezoni mwa Jamii, ili nao waweze kuonja na kuguswa na upendo wa Kristo kwa njia ya waamini. Uinjilishaji ni dhamana endelevu kwa Wakristo wa nyakati zote kutokana na dhamana waliyojitwalia wakati wa Sakramenti ya Ubatizo na kuimarishwa kwa Kipaimara kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Kristo ambaye ndiye kiini cha Injili na Imani inayotangazwa na kushuhudiwa na waamini. Kila mwamini anachangamotishwa na Mama Kanisa kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa.

Kardinali Filoni anapenda kuwahimiza Maaskofu na wadau wote wa Uenezaji wa Injili kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano; kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa, hasa zaidi kwa njia ya huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Watawa wanahamasishwa kuwa ni mfano bora wa maisha na tunu za Kiinjili kwa kuishi kikamilifu Mashauri ya Injili.

Waamini katika ujumla wao, wasimame kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu; wawe ni watetezi wa tunu msingi za maisha ya ndoa na familia kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao adili na manyofu; daima wakijitahidi kujenga na kuimarisha Jamii inayosimikwa katika misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati!







All the contents on this site are copyrighted ©.