Mshikamano wa upendo katika kupambana na majanga asilia duniani!
Shirika la Misaada la Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania, Manos Unidas, ambalo kwa
miaka mingi limekuwa mstari wa mbele katika kugharimia miradi ya maendeleo endelevu
pamoja na kusaidia watu kupambana na majanga asilia hususan katika nchi changa zaidi,
hivi karibuni limezindua kampeni ya mshikamano wa upendo miongoni mwa wananchi wa
Hispania ili kuchangia katika mfuko wa mshikamano na kilele cha kampeni hii ni hapo
tarehe 13 Desemba 2013. Katika kipindi
chote hiki, waamini na wananchi wenye mapenzi mema wanahamasishwa kuwasha moto wa
mshikamano kwa kuchangia kwa hali na mali. Kampeni hii inaendeshwa pia kwa kutumia
njia za mitandao ya kijamii ambayo imekuwa na ufanisi mkubwa katika kampeni mbali
mbali za kimataifa. Manos Unidas linawahamaisha waamini na watu wenye mapenzi
mema kutambua kwamba, kwa ushiriki na msaada wao wa hali na mali wanaweza kusaidia
kuleta mabadiliko msingi katika Jamii, ili kujenga dunia inayosimikwa katika msingi
ya haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati. Kutokana na changamoto mbali mbali
zinazoendelea kusababisha majanga na maafa makubwa katika maisha ya mwanadamu, Jamii
inachangamotishwa kufanya kazi kwa njia ya ushirikiano wa dhati, kwa ajili ya ustawi,
maendeleo na mafao ya wengi: kiroho na kimwili.