2013-12-02 09:26:12

Waamini wako katika hija ya kuelekea Yerusalemu mpya, mahali ambapo sura ya Mungu imeonekana na sheria kutangazwa!


Baba Mtakatifu Francisko katika tafakari yake, Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro amewakumbusha waamini kwamba, Kanisa limeanza Mwaka Mpya wa Liturujia, hija inayofanywa na Watu wa Mungu wakiongozwa na Yesu Kristo mchungaji mkuu katika utimilifu wa Ufalme wa Mungu. Ni hija inayofanywa na Mama Kanisa katika wito na utume wake, Familia ya binadamu wote; watu kutoka katika tamaduni na maendeleo mbali mbali kuelekea katika utimilifu wa nyakati!

Ni hija ya kiulimwengu kuelekea Yerusalemu mahali ambapo sura ya Mungu imefunuliwa na Sheria kutangazwa kwa watu wake. Yesu Kristo ni utimilifu wa ufunuo wa Mungu, ni Neno wa Mungu aliyefanyika mwili; kiongozi wa hija ya watu wa Mungu anayewaonesha mwanga unaoelekeza kwenye haki, amani na utulivu. Hakutakuwa tena na vita wala misigano! Baba Mtakatifu anasema, hii ni hija ya matumaini na amani inayobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwamba, ni hija endelevu katika maisha ya mwamini.

Kipindi cha Majilio ni wakati wa matumaini yasiyodanganya kamwe, kwani Mwenyezi Mungu ni mwaminifu katika ahadi zake. Bikira Maria ni mfano na kielelezo cha hija ya maisha, aliyebeba ndani ya moyo wake matumaini; na tumboni mwake tumaini la Neno wa Mungu aliyefanyika mwili, yaani Yesu Kristo. Utenzi wa Bikira Maria anasema Baba Mtakatifu ni wimbo wa mahujaji wanaotumainia: nguvu na huruma ya Mungu.

Mara baada ya Sala ya Malaika wa Bwana, Baba Mtakatifu Francisko aliwakumbuka wagonjwa wa Ukimwi sehemu mbali mbali duniani, lakini kwa namna ya pekee, watoto wanaoonja uwepo wa Mama Kanisa kwa njia ya Wamissionari na wahudumu wa Sekta ya Afya. Baba Mtakatifu amewaombea madaktari na watafiti waweze kufanikisha kazi yao na kwamba, kila mgonjwa aweze kupata huduma na asiwepo anayetengwa bila kupata tiba anayohitaji.







All the contents on this site are copyrighted ©.