2013-12-02 07:46:51

Shirikisheni vijana wa kizazi kipya katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi!


Shirikisho la Wakuu wa Shirika la Wayesuit Barani Afrika katika Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani, kwa mwaka 2013 linaitaka Jumuiya ya Kimataifa kuwahusisha vijana wa kizazi kipya katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi, kwa kuwajengea uwezo, tunu msingi za kiutu, kijamii na kimaadili pamoja na kuwafahamisha umuhimu wa mchango wao katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi. Hadi kufikia mwaka 2012 kulikuwa na jumla ya vijana million mbili nukta moja waliokuwa wanaoishi na virusi vya Ukimwi sehemu mbali mbali za dunia.

Mtandao wa mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi wa Wayesuit Barani Afrika, AJAN anasema Padre Michael Lewis, Rais wa Shirikisho la Wakuu wa Shirika la wayesuit Barani Afrika kwamba, wana amini kuhusu ufanisi unaoweza kupatikana katika elimu makini inayotolewa na AJAN Barani Afrika katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi; elimu inayotolewa shuleni na kwenye taasisi za elimu.

Vijana wanatambua kwamba, kampeni ya kinga dhidi ya Ukimwi bado haijafanikiwa sana, kwa mantiki kwamba, huu ni wimbo ambao kwa sasa hauna tena msikilizaji kwani umezoeleka masikioni mwao na watu wanaendelea kutumbua maisha kana kwamba, hakuna kinachoendelea duniani kuhusiana na Ukimwi! Wajesuit wanasema, kuna hja ya kuonesha kipaji cha ugunduzi kwa kuwashirikisha vijana wenyewe katika kampeni dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi.

Vijana waweze kuwa na mawazo pevu na nyenzo za kupambana na Ukimwi, kwa kuwajibika wanapofanya maamuzi ya maisha, kuwaonesha jirani zao upendo na huruma pamoja na kufanya maamuzi machungu ya kutaka kubadilika kitabia! Udhibiti wa maambukizi mapya ya Ukimwi uguse mahitaji ya mtu mzima; mahusiano kati ya mtu na mtu na kati ya mtu na Muumba wake. Vijana wawe na mitindo mipya ya maisha kwa kufahamu na kuzingatia mafundisho yanayotolewa na Mama Kanisa.








All the contents on this site are copyrighted ©.