Kanisa la Nyumbani! Familia iwe ni daraja la kwenda mbinguni!
“Ndoa inapaswa kuheshimiwa na watu wote, na haki zake zitekelezwe kwa uaminifu”. Ebr.
13:4a. Mpendwa msikilizaji, neno hili elekezi, litatuongoza katika tafakari zetu
zote za Kipindi chetu hiki cha Kanisa la Nyumbani. Kukuletea kipindi hiki, ni mimi
Padre Pambo Martin Mkorwe OSB kutoka Abasia ya Roho Mtakatifu Mvimwa – Sumbawanga,
Tanzania.
Mababa wa
Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, wanatutafakarisha juu ya Familia kama Kanisa la nyumbani.
Mafundisho ya imani yetu yanatuelekeza kwamba, Kanisa ni Sakramenti ya jumla ya ukombozi.
Ni kwa namna hiyohiyo,Familia ya Kikristo ambayo ni Kanisa la nyumbani, nayo tunaitazama
kama Sakramenti, yenye lengo lilelile la kumkomboa mwanadamu mwili na roho.
Hapa,
tunataka kusema, familia ziwe ni chombo cha kumuunganisha mwanadamu na mwanadamu mwenzake
na hatimaye mwanadamu huyu aunganike na Muumba wake. Kifupi tunataka kusema FAMILIA
ZETU ZIWE DARAJA YA KWENDA MBINGUNI.
Katika mfululizo wa vipindi vyetu “Kanisa
la Nyumbani”, tutatafakari kwa kina juu ya maana, hadhi, uzito na wajibu wa kila mmoja
katika kulijenga Kanisa la nyumbani. Mama Kanisa Mtakatifu anatualika kuienzi tunu
hii ya maisha ya familia, ili kutoka kwayo, Kanisa lizidi kusitawi na jamii nzima
ya mwanadamu iendelee kujengwa katika roho ya utu na heshima kwa Mungu.
Tunapoongea
juu ya familia katika Kanisa, moja kwa moja tunagusa suala msingi la Sakramenti ya
ndoa. Kristo Yesu, aliinua ndoa kuwa sakramenti, na akaesema “alichokiunganisha Mungu,
mwanadamu asitenganishe”. Kwa maneno hayo ndipo haswa alipothibitisha misingi na hadhi
ya agano la ndoa. Muasisi wa Sakramenti ya ndoa ni Mungu mwenyewe.
Kabla hatujazama
ndani kabisa ya mada yetu; ni vema sote tujue kwamba, ndoa ni wito. Humo wanaingia
tu wale walioitwa katika maisha ya ndoa. Ni Mungu mwenyewe ndiye anayeita na sisi
wanadamu kwa unyenyekevu na imani, tunaitika wito huo na kukubali wajibu zake; yaani
kudumisha upendo, kuzaa watoto na kuwatunza. Na ni katika kuupokea wito huo na wajibu
zake ndipo tunapolijenga KANISA LA NYUMBANI.
Kwa vile Sakramenti ya ndoa ni
wito, ni vema kuupokea wito huu kwa umakini mkubwa. Na kisha kuupokea wito huu kama
ilivyo kwa miito mingine, ni vema kuendelea kuuitika kila siku kwa njia ya kuomba
neema ya udumifu, kutimiza wajibu na kudumisha upendo wa kujisadaka kwa ajili ya mwenzi
na kwa ajili ya usitawi wa familia.
Baada ya kuuadhimisha mwaka wa Imani, kazi
itakayobaki mbele yetu, ni kuitambua kwa dhati na kuiimarisha misingi ya Kanisa. Na
moja ya tunu kubwa za Kanisa letu ni MAISHA YA NDOA NA FAMILIA. Kwa roho ya kichungaji,
tunapenda Kanisa la nyumbani liendelee kulishwa na kuimarishwa, kwa neno, sakramenti
na mafundisho mbalimbali, ili kweli usitawi wake, uakisi usitawi wa Kanisa zima la
Mungu.
Katika nyakati zetu hizi, ambapo Kanisa linapata changamoto nyingi kutokana
na ubaridi wa watu katika kupokea na kutunza wito wa ndoa; na kwa upande mwingine
changamoto ya mambo mbalimbali yanayoharibu uzito na unadhifu wa Kanisa la nyumbani;
tunaungana na Baba Mtakatifu kuwaalika watu wote “MSIOGOPE KUJENGA FAMILIA”. Watu
wengi kwa sababu ya uwoga, na pengine ubinafsi na uchoyo, hawapendi kujenga familia.
Hawapendi kuzaa watoto kwa kisingizio cha gharama, au hakuna muda wa kuwatunza. Au
wengine wataona watoto ni mzigo na karaha.
Tukiacha wajibu huo tuliopewa na
Mungu, Kanisa letu tutamwachia nani? Sote tuone kwamba TUNAWAJIBU WA KULIJENGA KANISA
LA SASA LA LA KESHO. Tunashiriki katika kulijenga Kanisa la kesho kwa kuwaandaa watu
wema, wenye kumjua na kumpenda Muumba wao na hivyo kumtumikia kwa njia ya Kanisa lenye
msingi katika familia bora.
Kipindi kijacho tutaendelea kwa kutafakari juu
ya maandalizi ya kuupokea wito wa ndoa. Kwa vile ndoa ni wito, anayeupokea anapaswa
kujiandaa vizuri kisaikolojia, kiroho na kijamii, ili tangu mwanzo ajue kwamba anapokea
wajibu mkubwa na wa maana sana. Tunafanya hivyo ili, isitokee kwamba mtu anaangukia
mahali ambaposio wito wake. Mtu anayeishi wito usio wa kwake, atateseka na kutesa
wengine; na hatimaye atakosa mastahili.
TUSIWE PEKE YETU, TUMHUSISHE MUNGU
KATIKA WITO NA MAISHA YA NDOA. Tunaendelea kuwaombea wote ambao tayari wapo katika
maisha ya ndoa na familia, Mungu mwenyewe aliyewajalia wito huo, kwa msaada wa neema
zake awasaidie kuuishi vema, ili yeye mwenyewe atukuzwe na wanadamu tuokolewe. BIKIRA
MARIA MALKIA WA FAMILIA – UTUOMBEE. Padre Pambo Martin Mkorwe, OSB.