Vipaumbele vya AMECEA kwa Mwaka 2014- 2016: Familia, Vijana na Majadiliano ya kidini
Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA katika
mkutano wake uliohitimishwa hivi karibuni katika mikakati yake ya kichungaji kwa Mwaka
2014 - 2016 limeamua kutoa kipaumbele cha kwanza kwa: familia, vijana na majadiliano
ya kidini, ili kujenga na kuimarisha tunu msingi za maisha ya kifamilia; kutoa matumaini
kwa vijana ambao ni jeuri ya Kanisa na kukoleza misingi ya haki na amani kama sehemu
ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya.
Familia inapewa kipaumbele cha kwanza kwa
kuzingatiwa kwamba, Baba Mtakatifu Francisko ameitisha Sinodi Maalum ya Maaskofu ili
kujadili na kufanya tafakari ya kina kuhusu: fursa, changamoto na kinzani zinazojitokeza
katika maisha ya ndoa na familia kwenye ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi
na teknolojia mintarafu dhamana ya Uinjilishaji.
Nchi za AMECEA zinapenda kutoa
matumaini kwa vijana kwa kukazia mikakati ya kichungaji kwa vijana kwa kukazia Utume
wa Biblia na malezi ya vijana kwenye vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu, ili vijana
waweze kulifahamu na kuliishi Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha yao ya ujana.
AMECEA inaandaa mpango mkakati utakaotumiwa na Nchi wanachama.
AMECEA katika
mikakati yake ya kichungaji kwa kipindi cha miaka miwili, inapenda kukazia umuhimu
wa majadiliano ya kidini ili kujenga na kuimarisha haki, amani na utulivu, kwa kuzingatia
kwamba, Jamii ya leo ni mkusanyiko wa watu wenye dini na imani mbali mbali, wanaopaswa
kuheshimiana, kupendana na kusaidiana kwa hali na mali katika hija ya maisha yao hapa
duniani. AMECEA inapenda kuwaelimisha waamini wake ili waweze kufahamu pia imani za
dini nyingine ili kuheshimiana na kuthaminiana hata katika utofauti.
Wakati
huu Jumuiya ya Kimataifa inaposhuhudia athari za mabadiliko ya tabia nchi katika maeneo
mbali mbali ya Afrika, AMECEA inasema kwamba, kuna haja kwa Kanisa kuendelea kuhimiza
utunzaji bora wa mazingira pamoja na ushiriki mkamilifu wa waamini walei katika maisha
na utume wa Kanisa kama sehemu ya mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu.