2013-11-30 10:49:26

Majaribio ya kwanza ya chanjo ya Ukimwi kwa watoto wenye virusi vya Ukimwi yaonesha mafanikio!


Jumuiya ya Kimataifa kila mwaka tarehe Mosi, Desemba, inaadhimisha Siku ya Ukimwi Duniani. Kwa mwaka huu, Siku hii inapambwa na matumaini ya kupatikana kwa chanjo ya watoto wenye virusi vya Ukimwi, iliyofanyiwa majaribio kwa watoto kumi katika Hospitali ya Bambino Gesu, inayoendeshwa na kumilikiwa na Vatican.

Taarifa kutoka Hospitali ya Bambino Gesu inasema kwamba, majaribio haya yamefanywa kwa kipindi cha miaka miwili kwa watoto waliokuwa na maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi na matokeo yake kuchapishwa kwenye Jarida la "Plos One", ili kutoa mwanya kwa mabingwa na wataalam wa afya kuweza kuangalia mafanikio haya. Majaribio haya yamefanywa kwa watoto ambao walikuwa wameambukizwa Ukwimwi tangu walipozaliwa na Mama zao.

Upatikanaji wa chanjo hii ni hatua muhimu sana katika mchakato wa kupunguza matumizi ya dawa za kurefusha maisha zinazotolewa kwa watoto walioathirika na ugonjwa wa Ukimwi. Taarifa inaonesha kwamba, chanjo hii ni mchanginyiko wa dawa kadhaa zinazodhibiti ongezeko la Virusi vya Ukimwi na hivyo kuuwezesha mwili kujijenga kinga yake. Pamoja na mafanikio hayo dawa hii bado inaonekana kuwa na madhara kwa watoto kuwa na kikohozi cha muda mrefu.

Watoto wanaozaliwa wakiwa wameambukizwa Virusi vya Ukimwi wanaweza kuanza kupata chanjo hii tangu mwaka wao wa kwanza na wataendelea na dawa hizi katika maisha yao yote! Dawa hii inaweza kusaidia kupunguza gharama za ununuzi wa dawa za kurefusha maisha pamoja na miundo mbinu inayohitajika kwa ajili ya tiba hii.







All the contents on this site are copyrighted ©.