2013-11-29 07:17:27

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio


Ni mara nyingine tena mpendwa msikilizaji wa Neno la Mungu, kipindi tafakari masomo Dominika. Kwa hakika Neno tunalolitafakari si Neno la kawaida bali ni Kristu mwenyewe mkate wa uzima wa mbinguni. RealAudioMP3
Ni mkate utupao uzima. Tunapenda kumshukuru Mungu kwa kutuwezesha kumaliza mwaka wa Kanisa na sasa Dominika hii tunaanza mwaka mpya wa Kanisa, yaani mwaka A Dominika ya kwanza ya Kipindi cha Majilio.
Mpendwa msikilizaji, katika kipindi cha Majilio, Mama Kanisa daima apenda kutukumbusha ujio wa Bwana Masiha, kwamba Bwana hakuja mara moja tu, bali anakuja kwetu siku zote, wakati wa raha na taabu. Ndiyo kusema yuko katikati yetu, yuko katika Kanisa, yuko kati ya wale wanaotangaza Injili na kuishi maisha ya upatanisho na amani.
Masiha anapokuja mara zote na kukaa nasi anatudai mabadiliko ya ndani yaani maisha yetu, tunaitwa kuendana na ujio wake. Tunaitwa kubadili tabia zetu na mienendo yetu. Ndiyo kusema tunaalikwa kutayarisha njia ya Bwana, kutayarisha kuzaliwa kwa Masiha. Hali hii daima yatupa furaha inayotusaidia kujiandaa kwa ajili ya ujio wa pili ambapo Bwana Masiha wetu atakuja kama Hakimu mwenye haki na si kama Mtoto Emanueli.
Mpendwa mwana wa Mungu, tunaalikwa na tunapaswa kuwa tayari kwa ajili ya ujio kama ambavyo masomo ya Dominika hii ya I ya Majilio yanavyotufundisha. Tunapata kutafakari masomo yetu ya Dominika hii tukiongozwa na kauri mbiu ya Kesheni na kusali maana hamjui siku wala saa atakayokuja Mwana wa mtu. Mwana huyu wa mtu anakuja kuanzisha dunia mpya, na Yerusalemu kutakuwa kitovu cha ulimwengu.
Kumbe, ujio wa Masiha ni ujio wa nuru, ni kuwaweka watu pamoja wakiielekea Yerusalemu mpya ya mbinguni. Injili ya Matayo ndiyo Injili ambayo itaongoza kipindi hiki cha Majilio na mwaliko utakuwa ni kukesha na kusali, kutenda matendo ya huruma na mapendo na kushika vema maagano yetu katika hali ya kila mmoja wetu.
Mpendwa msikilizaji, sehemu ya Injili ya Dominika hii yaani kutoka katika, Mt. 24:37-44 inasimikwa katika sura hiyohiyo ya 24 aya za kwanza, ambapo wanafunzi wanamwonesha Masiha, majengo na mahekalu mbalimbali, wakifikiri ni ya maana sana kwake , na Masiha atawaambia haya yote ni ubatili mtupu na yatabomolewa na hakuna kitakachosalia! Habari na maneno haya ni ya kieskatolojia, yaani yazungumza habari za mwisho wa maisha yetu hapa duniani.
Masiha akisha kuwaambia hilo baadaye atakuwa katika mlima wa mizeituni na hapo tena wanafunzi wake watamwuliza faraghani wakisema haya yatatukia lini? Basi Bwana ambaye hafuati vionjo, bali hufundisha kilicho cha kweli, atatoa jibu tofauti na udadisi wao, ndiyo kusema jibu ambalo latufaa sisi hivi leo na kwa wakati ujao. Anawapa jibu akitoa mfano wa gharika kuu la Noa na mwisho atasema, BASI KESHENI KWA MAANA HAMJUI SIKU WALA SAA.
Mpendwa msikilizaji, je jambo lililowapata watu wakati wa Noa laweza kutokea hivi leo? Natumai yawezekana! Ndiyo kusema, tukijaribu kufanya utafiti katika Neno la Mungu, tunaona Bwana akisema, maana nyakati hizo wakati kabla ya gharika watu walikuwa wakila na kunywa, wakioa na kuolewa na mpaka Noa anaingia katika safina hawakuwa na habari isipokuwa wachache.
Mambo ya ulevi, kuoa kusikokuwa katika mpango wa Kimungu, kutumbua na kula pasipo kuwajali maskini ni mambo ya kila siku katika jamii zetu, na hivi gharika la Nuhu kwa namna tofauti linakuja kila siku! Hatuko mbali nalo!
Angalia vifo vya watoto na watu wazima kwa sababu ya kukosa matibabu na zaidi sana uaminifu. Angalia uwepo wa watoto ambao tunawaita “watoto wa mitaani”, watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi, angalia ugomvi, vita na machafuko ya kidini na madhulumu mbalimbali. Haya yote ni magharika ambayo yanapelekea jamii na maisha yetu kuporomoka.
Mpendwa mwana wa Mungu, bado tunayo nafasi ya kupambana kinyume na magharika haya, na kwa hakika ni kujitwalia siraha za mwanga, nikujikabidhi mikononi mwa Masiha anayekuja kuleta amani na utulivu katikati yetu. Kumbe ujumbe wa Neno la Mungu katika Dominika hii kama tulivyokwishasema yaani Kesheni kila siku na kusali kwa maana hamjui siku wala saa ni wa kweli kwa wakati wetu.
Kukesha katika maandalizi ni ile hali ya kujikabidhi mikononi mwa Mungu tangu Dominika ya I ya Majilio mpaka Sherehe ya Yesu Kristu Mfalme. Ni kuweka daima mbele, masilahi ya jumuiya zaidi ya masilahi yangu binafsi. Bwana akisonga mbele katika mafundisho yake katika Dominika hii anaweka tena mfano mwingine kuhusu siku ya mwisho akisisitiza maandalizi ya dhati, akisema, wanawake wawili watakuwa wanasaga na mmoja atatwaliwa na mwingine ataachwa! Bwana ataka kusema kuwa hata katika maisha ya kawaida ya kila siku ni lazima kukesha. Ndiyo kusema tukiwa barabarani tukeshe, tukiwa kondeni tuziimbe sifa za Bwana na kuzitaraji daima fadhili za Bwana.
Mpendwa msikilizaji, usikubali kupoteza muda hata kidogo, daima ishi kwa kugawa na kuwashirikisha mapendo ya Mungu watu wote. Nikienda kuangalia historia ya Mtakatifu Gaspari mwanzilishi wa Shirika la Wamissionari wa Damu Takatifu, katika maisha yake alijitahidi kuipanua siku yake yaingie mawazo na matendo yake yote mema. Huu ni mwujiza, yaani siku ya masaa ya 24 inapanuliwa kwa ajili ya mapendo, na huko ndiko kuishi utayari wa kumpokea Masiha. Mtakatifu Gaspari alifuata nadharia ya “Elasticity ya mapendo”!
Mpendwa msikilizaji, tunarudia kwa ajili ya kukaza mafundisho, hivi kukesha kwaweza kuwa na maana gani tena? Ni kuhakikisha nafasi zote alizotupa Mwenyezi Mungu, tunazitumia vema. Nafasi zenyewe ni kutunza maisha ya sala, kuwajibika katika kazi, katika ndoa, katika upadre na maisha ya kitawa. Bwana wetu Yesu Kristu yuko daima katika nafasi hizo akitaka kutujaza furaha kamilifu. Kazi kubwa kumbe ni kuwa macho kuona ujio wake katika maisha hayo.
Mpendwa msikilizaji Mt Paulo anatupa tumaini akisema, wokovu wetu unakaribia na usiku unakwisha na mchana unaingia, tutupilie yote yatuleteayo aibu, tujitwalie siraha za mwanga. Anasisitiza kurudi katika ubatizo wetu na kutenda kadiri ya ubatizo, kuachana na matendo ya kipagani, yaani ulafi, ujeuri, rushwa, ufisadi wa mali ya umma na mambo kama hayo.
Mpendwa msikilizaji, ninapenda kukukumbusha kuwa mkristo ni mtu mwenye kuzitarajia siku za usoni kwa furaha, kwa sababu lengo la maisha yake siyo kuishi hapa duniani, bali ni kuufikia uhai usioharibika, yaani uzima wa milele. Mkristo anaishi hapa duniani akijiweka tayari kukutana na Bwana wake ambaye siku ile ya mwisho atamwalika aingie katika raha ya milele na kuishi naye daima.
Kumbuka kuwa tukio la kurudi ghafla kwa Masiha halimtishi mtu, ingawa hofu kidogo yapaswa kuwepo! Kwa nini halitishi, ni kwa sababu mtu akiwa tayari katika maisha yake basi siku ya mwisho ni kumalizia matayarisho yake ambayo yako tayari! Huyu anayejiweka tayari siku zote anayohamu daima akisubiri siku hiyo kwa furaha.
Basi mpendwa tupilia mbali vinyago ulivyonavyo na matunguli ya kiroho ili ukae mkao wa kumpokea Mwumba wako anapokuja kila siku na siku ya mwisho.

Ninakutakia majilio njema na mwanzo wa mwaka wa Kanisa wa furaha. Tumsifu Yesu Kristo na Bikira Maria.

Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.