Kijiji cha Matumaini ni kielelezo cha Injili ya Furaha na Matumaini kwa watoto walioathirika
kwa virusi vya Ukimwi
Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa Kitume, Injili ya Furaha, anawaalika
waamini na watu wenye mapenzi mema kumwiga Kristo aliyejifananisha na watu wadogo
wanaohitaji msaada, jambo ambalo ni changamoto kubwa katika ulimwengu wa utandawazi
unaoelemewa zaidi na ubinafsi na hali ya mtu kujitegemea, kiasi hata cha kushindwa
kuwekeza katika mchakato wa kuwasaidia wanyonge na wale wanaosukumizwa pembezoni Jamii
kuonja fursa mbali mbali zinazotolewa katika maisha.
Kijiji cha Matumaini
kinachomilikiwa na kuendeshwa na Shirika la Masista Waabuduo Damu Takatifu ya Yesu
kwa ajili ya watoto yatima na walioathirika na ugonjwa wa Ukimwi, kilianzishwa kunako
mwaka 2002 katika harakati za kusaidia kuwajengea matumaini watoto waliokuwa wameathirika
kwa ugonjwa wa Ukimwi. Padre Vincent Boselli muasisi wa Kijiji cha Matumaini katika
mahojiano na Radio Vatican anabainisha kwamba, Kijiji cha Matumaini kimepiga hatua
kubwa katika kuwasaidia waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi, Kanda ya Kati nchini Tanzania.
Katika
mikakati yao kwa watoto walioathirika na Ukimwi, walianza kuwapatia dawa za kurefusha
maisha na kwamba, watoto watatu wa kwanza kabisa hadi leo hii bado wako hai na wanaendelea
na masomo ya shule ya Sekondari.
Kijiji cha Matumaini kimeanzisha na kuendesha
kampeni ya kudhibiti maambukizi ya virusi vya Ukimwi kutoka kwa Mama kwenda kwa mtoto
wakati wa kuzaliwa na kunyonyesha na kuna mafanikio makubwa, kwani idadi ya watoto
wanaozaliwa pasi na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi wameongezeka maradufu kwenye Kijiji
cha Matumaini.
Hadi sasa wanawasaidia watoto wenye Virusi vya Ukimwi ambao
si yatima na wanaendelea kutunzwa na wazazi wao. Watoto hawa wanapewa huduma nje ya
Kijiji cha Matumaini na kwamba, kuna idadi kubwa ya watu walioathirika na Virusi vya
Ukimwi wangependa kupata huduma kutoka kwenye Kijiji cha Matumaini, lakini Padre Vincent
anasema, inashindikana kuweza kuwahudumia watu wote hawa ingawa pia ni vigumu kuwashauri
kwenda kupata huduma sehemu nyingine.
Kwa hakika, Kijiji cha Matumaini ni
kielelezo cha Injili ya Furaha na Matumaini kwa watoto walioathirika kwa ugonjwa wa
Ukimwi, Kanda ya Kati, nchini Tanzania.