2013-11-27 08:47:42

KAICIID yaanzisha ushirikiano na mashirika ya kimataifa ili kukoleza ari na moyo wa ushirikiano na majadiliano miongoni mwa waamini wa dini mbali mbali!


Kituo cha Majadiliano ya Kidini na Kitamaduni cha Mfalme Abdullah Bin Aziz, kwa kifupi KAICIID, kilichohitimisha warsha ya siku mbili huko Vienna, Austria kinasema kwamba, kimeanzisha ushirikiano wa pekee na Mashirika ya Kimataifa na kwamba, kati ya Mashirika haya ni: Umoja wa Afrika; Taasisi ya Elimu ya Dini ya Kiislam, Shirika la Kimataifa la Sayansi na Utamaduni, Mfuko wa Skauti Kimataifa pamoja na Shirika la elimu, sayansi na utamaduni la Umoja wa Mataifa.

Kituo hiki kinapania pamoja na mambo mengine kuendeleza mchakato wa elimu na majadiliano ya kidini miongoni mwa waamini wa dini mbali mbali duniani ili kujenga mazingira ya amani, utulivu na maendeleo endelevu. Elimu miongoni mwa vijana wa kizazi kipya ni jambo ambalo linapaswa kupewa kipambele cha kwanza ili kujenga mahusiano thabiti ndani ya Jamii na kuepusha misimamo mikali ya kidini na kiimani, ambayo imekuwa ikisababisha majanga sehemu mbali mbali za dunia.

Kituo hiki kimekuwa ni chombo ambacho kinawaunganisha wasomi, watunga sera, viongozi wa kidini na wapenda amani ili kwa pamoja kuweza kujadili mambo msingi na tete yanayomzunguka mwanadamu katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Ni matumaini ya viongozi wa kituo hiki cha majadiliano ya kidini kwamba, utekelezaji wa mikakati hii utaanza kufanyiwa kazi ili kujenga na kuimarisha ushirikiano na majadiliano na wadau mbali mbali.







All the contents on this site are copyrighted ©.