Ushuhuda wa Wakatekumeni, jinsi walivyoguswa hata wakaamua kumfuasa Yesu katika hija
ya maisha ya kiroho!
Katika Maadhimisho ya Kilele cha Mwaka wa Imani, Jumamosi jioni tarehe 23 Novemba
2013, Baba Mtakatifu Francisko amewapokea Wakatekumeni wanaojiandaa kupokea zawadi
ya Imani kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo, kwenye Ibada ya Neno la Mungu iliyofanyika
kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican.
Baba Mtakatifu amewapokea
Wakatekumeni 500 kutoka katika nchi 47 waliokuwa wamesindikizwa na wazazi wao wa ubatizo
pamoja na Makatekista wanaowandaa. Amewauliza maswali msingi na kile ambacho wanataka
kutoka kwa Kanisa nao wakajibu kwamba, wanataka imani ili waweze kuwa na maisha ya
uzima wa milele. Wakatekumeni ambao wameanza kutembea katika Mwanga wa Kristo mfufuka
wametakiwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Neno la Mungu; kumtambua na kujiaminisha
kwa Mwenyezi Mungu kwa njia ya maisha adili.
Haya ndiyo maisha ya Kanisa na
kwamba, tangu sasa Kristo ndiye atakayekuwa kiongozi wa maisha yao. Baba Mtakatifu
amewataka wazazi wa ubatizo na waamini katika ujumla wao, kuhakikisha kwamba, wanawasaidia
Wakatekumeni katika hija ya kumtafuta Kristo katika maisha yao.
Katika Ibada
hii, wakatekumeni wametiwa ishara ya Msalaba kwenye njia za fahmu, ili Kristo awalinde
kwa Ishara ya upendo wake mkuu, ili hatimaye, waweze kujifunza kumfahamu na kumfuasa.
Ibada hii imekamilika kwa Wakatekumeni kuingia kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro
lililokuwa limefurika kwa umati mkubwa wa watu wakati huu Mama Kanisa anapohitimisha
Mwaka wa Imani.
Wakatekumeni wameombewa ili waweze kupata msingi thabiti wa
imani yao ndani ya Kanisa, wakionesha umoja na mshikamano; wakiendelea kuutafuta uso
wa Yesu Kristo na kutekeleza mapenzi ya Mungu katika maisha yao. Waamini wawasaidie
Wakatekumeni katika hija yao ya kiimani, daima wakiwa makini kuguswa na shida pamoja
na mahangaiko ya jirani zao wanapojiandaa kuzaliwa upya kwa maji na Roho Mtakatifu.
Kabla
ya Ibada ya kupokelewa rasmi ndani ya Kanisa na Baba Mtakatifu, wakatekumeni walitoa
ushuhuda jinsi walivyobahatika kupata cheche za imani ya Kikristo walipokuwa vyuoni,
wakaguswa na Katekesi za kina zilizokuwa zinatolewa vyuoni humo; baadhi yao wamegundua
furaha ya imani kutokana na matatizo na changamoto za kuondokewa na wazazi wao; upweke
hasi uliopelekea jangwa la maisha ya kiroho; imani kwa Kristo kilikuwa ni kielelezo
cha furaha na zawadi ya uhai waliyokirimiwa.
Mmong’onyoko wa maadili na tunu
bora za maisha ya kiutu ni mambo yaliyochangia kwa baadhi yao kutafuta Mlango wa Imani,
ili kuweza kukutana na Yesu Kristo, Mwalimu na Bwana wa maisha! Ni watu waliotamani
kuonja fadhila ya imani, upendo na matumaini katika hija ya maisha yao! Baadhi ya
vijana wanasema, waliguswa kwa namna ya pekee na ushuhuda maisha ya Mwenyeheri Yohane
Paulo wa pili hasa miongoni mwa vijana, wakapenda na kuamua kumfuasa Kristo!
Baadhi
ya wakatekumeni wanasema, kwao imani ilikuwa ni kielelezo cha mwendelezo wa historia
ya uwepo wa Mungu kati ya watu wake, wakataka kuonja mang’amuzi haya mapya! Kati ya
wakatekumeni hawa, walionja Imani kwa njia ya tafakari ya Neno la Mungu, lakini matatizo
na changamoto za maisha, zimewafanya wengi kumkimbilia Kristo.
Kwa upande wao,
Makatekista wanasema, wameonja furaha ya imani kwa kuwasindikiza wakatekumeni katika
majiundo ya maisha yao ya Kikristo, kiasi cha kushirikishana tunu msingi za maisha
ya kiroho na watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia waliokuwa wanaishi Parokiani
mwao!