Wahudumieni wagonjwa kikamilifu kwa kutambua na kuthamini utu, utambulisho na mahitaji
yao msingi! Kamwe wasitengwe!
Wazee daima wamekuwa ni wadau wakuu katika maisha na utume wa Kanisa. Kuliko wakati
mwingine wowote katika historia ya mwanadamu, kuna haja kwa wakati huu, Kanisa kujitosa
kimasomaso kuwasaidia wazee katika Jamii kwa kuibua mbinu mkakati makini, kwani wazee
ni kielelezo cha hekima ya maisha, inayopaswa kurithishwa kwa wengine na kwamba, hawana
budi kuhusishwa kikamilifu katika utume wa Kanisa. Maisha ya kila mtu yana thamani
kubwa sana mbele ya Mwenyezi Mungu, licha ya tabia za kibaguzi zinazoweza kuoneshwa
na baadhi ya watu katika jamii.
Kutokana na maboresho ya huduma ya afya, watu
wameendelea kuishi kwa muda mrefu zaidi ikilinganishwa na ilivyokuwa kwenye karne
ya ishirini, hali ambayo inaambatana pia na shida pamoja na changamoto zake hasa magonjwa
ya mishipa ya fahamu yanayowandama wazee kwa asilimia kubwa, kiasi hata cha kupoteza
fahamu.
Magonjwa haya yanahitaji uwekezaji makini kutoka katika Jumuiya ya
Kimataifa hasa katika masuala ya tafiti, huduma na tiba muafaka kwa wagonjwa hao.
Familia inabaki kuwa ni mahali pa faraja na ukarimu kwa wagonjwa.
Ni sehemu
ya hotuba iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi, tarehe 23 Novemba 2013
alipokutana na kuzungumza na wajumbe wa mkutano wa XXVIII Kimataifa ulioandaliwa na
Baraza la Kipapa kwa ajili ya huduma kwa wafanyakazi wa sekta ya afya, uliohitimishwa
mjini Vatican.
Baba Mtakatifu anasema, wagonjwa hawana budi kuhudumiwa kikamilifu,
kwa kuheshimu na kuthamini utu, utambulisho na mahitaji yao msingi, bila kuwatenga
wale wanaowahudumia, ndugu, jamaa na wafanyakazi katika sekta ya afya. Yote haya yanawezekana
ikiwa kama kuna imani na hali ya kuheshimiana kati ya wadau mbali mbali. Kwa mwelekeo
huu, huduma kwa wagonjwa inayotolewa kwa weledi mkubwa inagusa pia ubinadamu wao,
vinginevyo, huduma kwa wagonjwa linakuwa ni jambo la mpito!
Baba Mtakatifu
anawahimiza wafanyakazi katika sekta ya afya kuendeleza huduma makini kwa wagonjwa
mintarafu mapokeo ya kitabibu, kwa kuboresha zaidi utu, uhuru na ukimya usiokuwa na
maana ambao wakati mwingine unawaandama wale wanaofanya kazi ya huduma kwa wagonjwa.
Baba Mtakatifu anawahimiza wafanyakazi hawa kuhakikisha kwamba, wanadumisha mwelekeo
wa kidini na maisha ya kiroho kwa wagonjwa, hali inayobaki hata pale mgonjwa anapopoteza
fahamu zake.
Baba Mtakatifu Francisko anawataka wahudumu katika sekta ya afya
kuendeleza huduma ya maisha ya kiroho kwa wazee wagonjwa wanaokabiliwa na magonjwa
ya mishipa ya fahamu, ili kuwasaidia kuendeleza uhusiano na majadiliano na Mwenyezi
Mungu kutoka katika undani wa maisha yao.
Baba Mtakatifu anahitimisha hotuba
yake kwa kuwatakia kheri na baraka wazee waliotawanyika sehemu mbali mbali za dunia.
Wafanyakazi katika sekta ya afya watambue pia kwamba, ni sehemu ya wadau wa Uinjilishaji
kwa njia ya sakramenti ya Ubatizo waliyoipokea. Kila siku ya maisha yao, wanapaswa
kuwa ni mashahidi wa Kristo katika sehemu mbali mbali za maisha ya mwanadamu na kwa
njia hii, watu wanaweza kumfahamu na kumpenda Kristo na Injili yake hasa miongoni
mwa vijana. Baba Mtakatifu amewaweka wajumbe hao chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira
Maria msaada wa wagonjwa.