Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican unaendelea kuyachangamotisha Makanisa ya Mashariki
kudumisha majadiliano ya kidini na kiekumene, Umoja na Ushuhuda wa imani katika matendo!
Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki hapo tarehe 22 Novemba 2013 limehitimisha
mkutano wake wa Mwaka uliofunguliwa tarehe 19 Novemba 2013 kwa kuwashirikisha wakuu
wa Makanisa kutoka Mashariki pamoja na viongozi waandamizi kutoka Vatican.
Wajumbe
wa mkutano huu wamepata fursa ya kupembua mawazo makuu yaliyojitokeza tangu Maadhimisho
ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican kuhusiana na Makanisa ya Mashariki hadi nyakati
hizi. Mkutano umeendeshwa katika hali ya utulivu na amani na hivyo kutoa fursa kwa
wajumbe kushirikishana mang'amuzi ya maisha na utume wa Makanisa ya Mashariki; kusikiliza
kwa makini na kuchangia kwa umakini mkubwa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Makanisa
ya Mashariki.
Waamini kutoka katika Makanisa haya wameathirika kwa namna ya
pekee na vita; ukosefu wa uhuru wa kuabudu, madhulumu na nyanyaso za kidini zilizopelekea
makundi makubwa ya waamini kuzikimbia nchi zao ili kusalimisha maisha yao. Waamini
hawa wakaonja upendo na huruma kutoka kwa waamini wa Makanisa yenye madhehebu ya Kilatini;
wakapewa nyumba za Ibada na kutambuliwa uwepo wao!
Licha ya tofauti ya Kanuni
na Sheria za Kanisa, wajumbe kwa pamoja wamepongeza utekelezaji wa maamuzi makuu yanayofanywa
kwa njia ya Sinodi za Mapatriaki, sanjari na mwendelezo wa majadiliano ya kina na
Khalifa wa Mtakatifu Petro, kama alivyofanya tarehe 21 Novemba 2013 kwa kuzungumza
na Mapatriaki, Maaskofu wakuu pamoja na wajumbe wa Mkutano wa Baraza la Kipapa kwa
ajili ya Makanisa ya Mashariki.
Wajumbe wa mkutano huu wameguswa kwa namna
ya pekee na Mafundisho juu ya Kanisa kama yalivyotolewa na Mababa wa Mtaguso Mkuu
wa Pili wa Vatican kwa kukazia majadiliano ya kidini na kiekumene ili kukuza na kudumisha
umoja katika tofauti; kwa kuendelea kusoma alama za nyakati; daima Makanisa ya Mashariki
yakijitahidi kujenga na kuimarisha umoja na Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Wajumbe
wamegusia pamoja na mambo mengine kuhusu halisi ya kitume, tatizo na changamoto ya
wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum; uwepo wa Wakristo Mashariki ya Kati
na changamoto zake pamoja na kuangalia umuhimu wa kuwa na vongozi wa Kanisa mahali
ambapo kuna makundi haya ili yaweze kupata huduma za maisha ya kiroho hata pale wanapokuwa
ugenini kwa kuzingatia kanuni, sheria na Mapokeo ya mahali wanapotoka.
Wajumbe
wameonesha umuhimu wa kujenga miundo mbinu kwa ajili ya huduma za kichungaji kwa waamini
wa Makanisa ya Mashariki mintarafu changamoto za Uinjilishaji Mpya, kwa kuzingatia
pia Mapokeo ya maisha ya kiroho na Liturujia ya waamini kutoka katika Makanisa yao.
Kuna haja ya kuendeleza majadiliano ya kiekumene miongoni mwa Wakristo kadiri ya utashi
wa Kristo, ili wote wawe wamoja chini ya Kristo Mchungaji mkuu, kwa kuendeleza ushuhuda
na mshikamano na Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Wajumbe wanasema, viongozi wa
Makanisa ya Mashariki waendelee kuongoza, kuadhimisha Liturujia na ufahamu wa Fumbo
la Kristo, mintarafu taalimungu na Kanuni ya Imani ya Costantinopoli. Makanisa ya
Mashariki na Magharibi kwa pamoja yanaendelea kuchangamotishwa kukuza na kudumisha
majadiliano ya kiekumene na kidini katika uhalisia wa maisha ya kila siku.
Wawe
ni mashahidi wa upendo wa Kristo katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu
na kwamba, wanahamasishwa na Mama Kanisa kuendeleza mchakato wa Uinjilishaji Mpya.