Wapendwa wanafamilia ya Mungu, karibuni kwa tafakari ya Neno la Mungu, inayotujia
tunapoadhimisha leo Sherehe ya Bwana wetu Yesu Kristo Mfalme. Mama Kanisa anatualika
tumtafakari Kristo ambaye ni Mfalme wa Ulimwengu na pia kielelezo halisi cha Mfalme
wa kweli ambaye ni tofauti na wafalme wa dunia hii.
Tofauti
na miaka mingine, kwa mwaka huu adhimisho hili la Sherehe ya Kristo Mfalme linaambatana
na hitimisho rasmi la Mwaka wa Imani. Hivyo ni nafasi nzuri kwetu kujikumbusha kuwa
Imani ya kweli ni ile ambayo inajengeka katika Kristo Mwenyewe ambaye atatupa tuzo
la kushiriki maisha katika ufalme wake wa mbinguni kadiri ile ambavyo tumejibidisha
kuiishi imani yetu na kwa jinsi tulivyomruhusu awe Bwana na Mtawala wa maisha yetu.
Kihistoria, sherehe hii ilianzishwa na Papa Pius XI mwaka 1925 akitaka kumtambulisha
Kristo kuwa ndiye mfalme wa kweli tofauti na wafalme dhalimu wa nyakati hizo, na kuwakumbusha
wanadamu kuwa amani, furaha, na upendo wa kweli kwa mwanadamu vinapatikana kwa kumruhusu
Kristo atawale maisha yetu. Mtawala yeyote wa dunia hii, pamoja na heshima halali
anazostahili kupewa, kamwe asitazamwe kuwa ndio ukomo wetu, bali mwanzo na ukomo wetu
ni Kristo Mwenyewe ambaye ni Bwana na Mfalme.
Tangu mwaka 1925 Sherehe
hii iliadhimishwa Jumapili ya Mwisho ya Mwezi Oktoba iliyotangulia Sherehe ya Watakatifu
wote hadi mwaka 1969 ambapo Papa Paul VI aliipa tarehe mpya na kuanza kuadhimishwa
katika Jumapili ya Mwisho wa Mwaka wa Kanisa hadi leo hii. Tunaiadhimisha Sherehe
hii Jumapili ya Mwisho wa Mwaka wa Kanisa kuashiria kuwa Kristo ni Mfalme wa Nyakati
zote atakayekuja mara ya pili kwa utukufu kuwahukumu wazima na wafu; huku tukitazamia
kuanza kipindi cha Majilio - ambapo tunatazamia ujio wa kwanza wa Kristo kama Masiha.
Maandiko
Matakatifu kutoka katika masomo ya Jumapili hii, yanatuongoza na kutusaidia kutafakari
kwa undani zaidi juu ya fundisho hili juu ya Ufalme wa Kristo na namna ambavyo Kristo
anavyojidhihirisha kuwa Mfalme wa pekee sana, tofauti na wafalme wa dunia hii, na
kutoa changamoto kwetu jinsi ya kushiriki maisha katika ufalme huo kwa kumruhusu Krito
atawale maisha yetu.
Injili ya leo inatupeleka mpaka Kalvari ambapo tunamwona
Kristo akiwa ameangikwa Msalabani, anathibitisha kuwa Yeye ni Mfalme na Bwana wa Uzima
hasa kwa kumwahidia Uzima wa Milele yule “mwizi aliyetubu” – ambaye ni yeye pekee
kati ya wale wote waliomzunguka pale Msalabani aliyeweza kukiri na kumshuhudia kuwa
hakika Kristo ni Mfalme.
Kristo anajitambulisha kuwa yeye ni Mfalme Mnyenyekevu
na asiyependa sifa wala makuu; kwa kutokuwa tayari kukidhi kiu ya wale waliomkejeli
na kumkashifu pale Msalabani kwa kumtaka jinsi ile ile alivyowaokoa wengine vivyo
hivyo ajiokoe mwenyewe. Aidha, anajidhihirisha kwetu kuwa ni Mfalme mwenye kusamehe:
akiwasamehe kuanzia wale waliokuwa wanamkashifu pale Msalabani, na zaidi sana yule
mwizi ambaye kwa hakika alipata wokovu hatua za mwishomwisho. Kristo anasamehe pasipo
kujali uzito wa dhambi bali anatazama uthabiti wa toba ya mtu.
Somo la
kwanza, linaeleza juu ya kutawadhwa kwa Mfalme Daudi ambako kunaambatana na tendo
la kupakwa mafuta. Ni kutoka katika Ukoo huu wa Kifalme ndipo anazaliwa Kristo Masiha
na ambaye ni Mfalme: tena Mfalme wa Mbingu na Dunia na wa Milele tofauti na alivyokuwa
Daudi na wafalme wengine wa dunia hii.
Katika Somo la Pili, Mtume Paulo
anamtambulisha kwetu Yesu Kristo Mfalme wa Milele, aliye asili ya vitu vyote, anayetukomboa
kutoka katika giza na kutuingiza katika nuru, kwake tunapata msamaha wa dhambi zetu,
tunapata amani kutokana na kifo chake Msalabani na kufunguliwa mlango wa mbingu kwa
ufufuko wake. Kristo ni mtangulizi wetu katika yote, na hivi tunayo kila sababu ya
kumshukuru Mungu!
Kutokana na utajiri huo tunaoupata kutoka katika masomo
ya leo, tunaona dhahiri kuwa Bwana wetu Yesu Kristo ni Mfalme wa pekee kwani: ni
Mfalme wa amani, wa haki, mwenye upendo kwa wote, mtumishi na sio mtumikiwa, mnyenyekevu
na si mpenda makuu, mwamuzi mvumilivu na mwenye huruma wala asiye mwepesi wa hasira;
kiongozi na si mwenye kuamuru tu, mwenye kusamehe na sio kulipiza kisasi; Mchungaji
na sio mpenda madaraka, anayehangaikia uzima na ustawi wa watu wote pasipo kuendekeza
ubinafsi, na ambaye ufalme wake ni wa nyakati zote.
Hivyo katika Jumapili
hii, tunapewa changamoto ya kufanya uchaguzi huru wa ama kumfuata Kristo Mfalme au
kinyume chake, yaani, kufuata ufalme wa mwovu shetani. Tutadhihirisha tu kuwa tunamfuata
Kristo Mfalme kwa maisha yetu, jinsi ambavyo tunaziishi hizo tunu njema zinazoutambulisha
ufalme wake.
Vinginevyo tutakuwa tumejisajili katika ufalme wa shetani
kama tutaruhusu maisha yetu yatawaliwe na matendo maovu kama vile: ubinafsi, chuki,
vita, kutothamini uhai, kupoteza ladha ya masuala yanayomuhusu Mungu, kutekwa na maendeleo
ya sayansi na teknolojia kwa kumsahau Mungu; utoaji mimba, ndoa za jinsia moja, uvunjifu
wa ndoa, ukosefu wa malezi bora katika familia, kuhalalisha dhambi na kutoona thamani
ya toba, unyanyasaji, uchu wa mali na madaraka, na mengine kama hayo tunayoyashuhudia
katika ulimwengu wetu wa leo.
Wapendwa wanafamilia ya Mungu, ninapenda
kuhitimisha tafakari hii kwa kumwalika kila mmoja wetu amshukuru Mungu kwa zawadi
ya mwanaye Bwana wetu Yesu Kristo – ambaye amemtuma ili atawale na kuongoza maisha
yetu, tunaposafiri kuelekea mbinguni. Aidha, tunapohitimisha leo adhimisho la Mwaka
wa Imani, tuendelee kujiombea sisi wenyewe, kwanza: msamaha kwa jinsi ambavyo mara
nyingi tumeisaliti imani yetu kwa kuishi kinyume na matakwa ya ufalme wa Kristo.
Pili,
tumwombe Mungu ili tudumu siku zote katika imani kwake. Tuwaombee wale wengine ambao
hawajapata bado kuisikia sauti ya Kristo na zaidi sana wale ambao wamejitenga na ufalme
wa Kristo ili wapate kurudi, na hatimaye, sote tuweze tena kuwa kundi moja chini ya
Mchungaji na Mfalme mmoja, Bwana wetu Yesu Kristo.
Tumsifu Yesu Kristo.
Na:
Pd. Kwene Alfred, Jimbo Katoliki la Musoma, Tanzania.