Rais Vjekoslav Bevanda akutana na kuzungumza na Papa Francisko mjini Vatican
Baba Mtakatifu Francisko, tarehe 22 Novemba 2013 amekutana na kuzungumza na Bwana
Vjekoslav Bevanda, Rais wa Baraza la Mawaziri nchini Bosnia na Erzegovina, ambaye
pamoja na ujumbe wake amekutana na Askofu mkuu Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican
aliyeambatana na Askofu mkuu Dominique Mamberti, katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje
na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.
Mazungumzo haya ambayo yamefanyika
katika hali ya urafiki, imekuwa ni fursa kwa viongozi hawa wawili kujadili pamoja
na mambo mengine hali halisi ilivyo nchini Bosnia na Erxegovina sanjari na kuanzisha
mchakato utakaoiwezesha nchi hii kuwa wazi zaidi kwa kusimama kidete kulinda na kutetea
haki msingi za binadamu pamoja na changamoto za athari za myumbo wa uchumi kimataifa.
Pande zote mbili zimeridhika kwa uhusiano uliofikiwa kati ya pande hizi mbili,
mintarafu itifaki ya mwaka 2006, ulioonesha umuhimu wa mshikamano na ushirikiano kati
ya Kanisa na Serikali kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi. Katika mazungumzo
yao wameangalia pia jinsi ya kutekeleza itifaki hii na jinsi ambavyo Kanisa Katoliki
linaweza kuchangia zaidi katika ustawi wa nchi yao.