2013-11-22 15:17:18

Rais Vjekoslav Bevanda akutana na kuzungumza na Papa Francisko mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, tarehe 22 Novemba 2013 amekutana na kuzungumza na Bwana Vjekoslav Bevanda, Rais wa Baraza la Mawaziri nchini Bosnia na Erzegovina, ambaye pamoja na ujumbe wake amekutana na Askofu mkuu Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyeambatana na Askofu mkuu Dominique Mamberti, katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.

Mazungumzo haya ambayo yamefanyika katika hali ya urafiki, imekuwa ni fursa kwa viongozi hawa wawili kujadili pamoja na mambo mengine hali halisi ilivyo nchini Bosnia na Erxegovina sanjari na kuanzisha mchakato utakaoiwezesha nchi hii kuwa wazi zaidi kwa kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu pamoja na changamoto za athari za myumbo wa uchumi kimataifa.

Pande zote mbili zimeridhika kwa uhusiano uliofikiwa kati ya pande hizi mbili, mintarafu itifaki ya mwaka 2006, ulioonesha umuhimu wa mshikamano na ushirikiano kati ya Kanisa na Serikali kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi. Katika mazungumzo yao wameangalia pia jinsi ya kutekeleza itifaki hii na jinsi ambavyo Kanisa Katoliki linaweza kuchangia zaidi katika ustawi wa nchi yao.







All the contents on this site are copyrighted ©.