2013-11-22 10:44:08

Mshikamano wa upendo na wananchi walioathirika kwa majanga asilia wakati wa kufunga Mwaka wa Imani mjini Vatican


Katika Maadhimisho ya Kilele cha Kufunga Mwaka wa Imani, Jumapili ijayo kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, waamini na watu wenye mapenzi mema watachangia sadaka itakayopelekwa nchini Ufilippini ili kusaidia watu waliokumbwa na majanga nchini humo, kama kielelezo makini cha mshikamano na watu wenye shida mbali mbali Mama Kanisa anapofunga rasmi Mwaka wa Imani.

Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum linasema kwamba, kunako Mwaka 2004 na Mwaka 2011 mchango kama huu ulikusanywa kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wa Asia Kusini waliokumbwa na Tsunami na baadaye wananchi wa Japan walipokumbwa na mafuriko yaliyosababisha maafa makubwa.

Msaada huu unasimamiwa na kuratibiwa na Utume wa Bahari kwa ajili ya nchi zilizoathirika kwa majanga asilia. Kanisa Katoliki kwa njia ya mashirika yake ya misaada linaendelea kuwafariji waathirika kwa hali na mali. Msaada huo pamoja na mambo mengine, utakuwa ni kielelezo halisi cha mshikamano wa dhati katika ujenzi wa makazi, ununuzi wa vifaa vya uvuvi na huduma ya elimu kwa watoto yatima na wale wanaoishi katika mazingira hatarishi.







All the contents on this site are copyrighted ©.