Bikira Maria ni Mama wa Matumaini! Je, bado taa ya matumaini inaendelea kuwaka katika
Monasteri?
Shamrashamra za kufunga Mwaka wa Imani sanjari na Sherehe za Kristo Mfalme zimeanza
kutimua vumbi mjini Vatican baada ya Baba Mtakatifu Francisko. Alhamisi tarehe 21
Novemba 2013 kuwatembelea na kusali pamoja na Wamonaki wa Shirika la Wakamadoli mjini
Roma.
Baba Mtakatifu aliongoza Ibada ya Masifu ya Jioni na baadaye Askofu
mkuu Rino Fisichella, Rais wa Baraza la Kipapa la uhamasishaji wa Uinjilishaji mpya
aliongoza Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu, kama changamoto kwa waamini kumkaribisha
Kristo katika hija ya maisha yao ya ndani.
Katika tafakari yake, Baba Mtakatifu
anasema, Bikira Maria alionesha upendo mkuu kwa Yesu na akajitahidi kutekeleza mapenzi
ya Mungu katika hija ya maisha yake hapa duniani, kiasi kwamba, akawa ni Mama wa Mkombozi
na Mwanafunzi amini wa Kristo, aliyejiaminisha mikononi mwa Mwenyezi Mungu, kielelezo
cha mtu mwenye matumaini thabiti.
Bikira Maria alikubali mpango wa Mungu katika
maisha yake tangu siku ile alipopashwa habari kwamba, atakuwa ni Mama wa Mungu. Hakufahamu
undani wa Fumbo la Umwilisho, lakini akalisubiri kwa moyo wa matumaini, hata siku
ile Masiha alipozaliwa katika hali ya umaskni, lakini hata katika mazingira kama haya,
hakukata tamaa, ingawa siku ile Yesu alipokuwa anatolewa Hekaluni, Wazee Simeoni na
Anna walimwambia kwamba, upanga utaingia moyoni mwake, ili yafunuliwe mawazo ya mioyo
mingi. Utume wa Bikira Maria katika historia ya ukombozi kwa kiasi fulani unafanana
na utume wa Yesu katika Fumbo la Ukombozi.
Baba Mtakatifu anasema, licha ya
magumu na changamoto zote hizi, bado Bikira Maria aliendelea kuwa ni mwanamke wa matumaini
aliyeyarutubisha kwa njia ya kusikiliza kwa makini Neno la Mungu; akalitafakari kwa
unyenyekevu na kulimwilisha kwa njia ya matendo ya huruma, pale mjini Kana, wanaharusi
walipotindikiwa na divai. Hapa akamtambulisha Yesu kuwa ni Mwalimu na Masiha. Bikira
Maria akayahifadhi matukio yote haya katika sakafu ya moyo wake mtakatifu. Mwanaye
mpendwa Yesu akaonekana kuwa kweli alama ya kusimama na kuanguka kwa wengi, kama ilivyokuwa
imetabiriwa.
Baba Mtakatifu anasema, Bikira Maria chini ya Msalaba akalitafakari
Fumbo la Pasaka kwa uchungu na kwa wale waliokata tamaa wangeweza kusema, hapa matumaini
ya Bikira Maria yalizimika kama kibatari! Lakini, Bikira Maria ni Mama wa Imani thabiti,
akaendelea kusadiki katika mpango wa Mungu bila kuyumba wala kuteteleka! Bahati mbaya,
binadamu wa leo anataka muujiza mara moja, hana tena subira ya kusubiri ile Alfajiri,
Siku ya kwanza ya Juma! Pale kaburini, taa iliyokuwa inawaka ilikuwa ni ya Mama Bikira
Maria, tumaini kwa familia yote ya binadamu.
Baba Mtakatifu Francisko anauliza,
Je, hata leo hii taa ya matumaini bado inawaka kwenye Monasteri?, Je, wanaendelea
kusubiri Mpango wa Mungu katika maisha yao? Bikira Maria aliyejipambanua katika historia
ya wokovu ni shahidi makini wa tumaini, anayewaenzi watoto wake wakati wa shida na
magumu; anawafariji pale wanapoonekana kana kwamba, yote yamekwisha!