2013-11-20 09:09:33

Mshikamano na wananchi wa Sardegna waliokumbwa na maafa!


Baba Mtakatifu Francisko amepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za maafa yaliyojitokeza Kisiwani Sardegna kutokana na mvua kubwa iliyonyeesha ikiambatana na upepo mkali na hivyo kusababisha watu zaidi ya 16 kupoteza maisha sanjari na uharibifu mkubwa wa mali. Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wenye mapenzi mema kuungana naye kwa sala kwa ajili ya waathirika na hasa zaidi watoto wanaoendelea kuteseka kutokana na janga hili.

Katika ujumbe uliondikwa kwa niaba yake na Askofu mkuu Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, Baba Mtakatifu anapenda kuwahakikishia wote walioguswa na janga hili uwepo wake wa karibu hasa kwa njia ya sala. Anawaalika watu wenye mapenzi mema kuonesha moyo wa mshikamano kwa waathirika wa mafuriko haya ambayo yamesababisha uharibifu mkubwa wa miundo mbinu.

Ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko umetumwa kwa Askofu Arrigo Meglio, Rais wa Baraza la Maaskofu Sarda, Kusini mwa Italia.







All the contents on this site are copyrighted ©.