2013-11-20 12:00:50

IMBISA inapania kuwa ni kielelezo cha mshikamano na umoja wa Kanisa kusini mwa Afrika!


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Kusini mwa Afrika, IMBISA katika mkutano wake wa kumi, uliohitimishwa hivi karibuni, limekazia umuhimu wa kujenga na kuimarisha mshikamano wa dhati miongoni mwa Maaskofu na Waamini ili kushuhudia Ukatoliki wao katika matendo.

Pamoja na mambo mengine, Maaskofu wa IMBISA wamejadili kuhusu maswali dodoso yaliyotumwa kwao kama sehemu ya Maandalizi ya Maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, itakayoadhimishwa mwezi Oktoba 2014 mjini Vatican.Maaskofu wamejadili kwa kina na mapana kuhusu changamoto, fursa na matatizo yanayozikabili familia kwenye Nchi za IMBISA na kuamua kwamba, kila Baraza la Maaskofu lianzishe Idara ya Familia itakayoundwa na Waamini walei pamoja na Mapadre kama sehemu ya mchakato wa kuendeleza tunu msingi za maisha ya kifamilia Barani Afrika.

Maaskofu wamekazia umuhimu wa Sakramenti ya Ndoa na kuwataka waamini kuacha mtindo wa ndoa za majaribio ambazo zinazodhohofisha kwa kiasi kikubwa heshima, heshima na uwajibikaji wa daima miongoni mwa watu wa ndoa. Waamini watambue maana ya Sakramenti ya ndoa katika maisha yao ya kiroho na kijamii, tayari kuanza mchakato wa ujenzi wa Familia kama Kanisa dogo la nyumbani, linalosali na kuhudumiana kwa upendo na ukarimu. Maaskofu wamekubaliana kimsingi kuanzisha vyama vya kitume vitakavyowasaidia wanandoa wapya kushauriana katika safari ya maisha yao ya pamoja.

Changamoto inayojitokeza kwa familia nyingi Kusini mwa Afrika ni ongezeko la familia tenge, zinazohudumiwa na mzazi wa upande mmoja; familia nyingi kwa sasa zinahudumiwa na wazee wenye umri mkubwa na kwamba, kuna wasichana wengi wanapata watoto kabla ya kufunga ndoa; hili ni kundi linalokabiliwa na hali ngumu ya maisha. Kuna ongezeko la watoto yatima na wale wanaoishi katika mazingira hatarishi kutokana na kuachwa na wazazi wao kwa ugonjwa wa Ukwimi. Tatizo hili linakwenda sanjari na ongezeko la wajane.

Maaskofu wa IMBISA wanasema mambo yote haya yanachangia kwa kiasi kikubwa kuzorota kwa misingi thabiti ya maisha ya ndoa na familia Kusini mwa Afrika. Mwaka 2014 ni Mwaka wa Familia kwa Jumuiya ya Kimataifa ni changamoto wanasema Maaskofu kutumia fursa hii kuimarisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia.

Maaskofu wanasema, IMBISA linapaswa kuwa ni jukwaa la majadiliano miongoni mwa Maaskofu na mahali pa kutajirishana kiroho, huku wakipania kusaidiana na kutaabikiana, licha ya tofauti za lugha zinazoweza kuonekana wakati mwingine kuwa kama kikwazo. Wanasema, wataendelea kusimama kidete kulinda na kutetea: mafao ya wengi, utu na heshima ya binadamu; utawala bora kwa nchi za SADC. IMBISA inapaswa kujenga na kuimarisha jukwaa la majadiliano ya kidini na Wakristo wa madhehebu mengine.

Maaskofu wa IMBISA wameonesha wasi wasi wao kutokana na kuzuka kwa vita nchini Msumbiji, hali ambayo inaweza kukwamisha juhudi za kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa. Mwishoni, Askofu Frank Nubuasah kutoka Botswana amechaguliwa tena kuwa Rais wa IMBISA; Makamu wake ni Askofu Lucio Andrice Mandula kutoka Msumbiji na Askofu mkuu Robert Ndlovu kutoka Zimbabwe amechaguliwa kuwa Katibu mkuu wa IMBISA.







All the contents on this site are copyrighted ©.