2013-11-19 09:45:13

Viongozi wakuu kutoka Makanisa ya Mashariki na Vatican wanakutana!


Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki, kuanzia tarehe 19 hadi tarehe 22 Novemba 2013 linafanya mkutano wake wa Mwaka, unaohudhuriwa na viongozi waandamizi kutoka Makanisa ya Mashariki pamoja na Vatican.

Wajumbe wanaendelea kuchambua mafundisho ya Kanisa tangu Karne ya Kumi na nne hadi kwenye Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na mchango wa Makanisa ya Mashariki katika ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kiulimwengu.

Makanisa ya Mashariki ni kielelezo cha umoja katika tofauti, kama changamoto ya kuendeleza mchakato wa Uinjilishaji mpya pamoja na kushirikiana imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Sheria za Makanisa ya Mashariki zilizochapishwa kunako mwaka 1990 ni matunda ya Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican yanayokwenda sanjari na mabadiliko katika Liturujia kwa Makanisa haya na mwaliko wa kuendeleza majadiliano ya kiekumene, ili wote waweze kuwa wamoja chini ya Kristo.

Makanisa ya Mashariki yanahimizwa kuendeleza Mapokeo ya Kimonaki kama sehemu ya mchango wake maalum kwa ajili ya ukuaji wa maisha ya kiroho na Kisakramenti, hasa kwa waamini kutoka kwenye Makanisa ya Mashariki wanaoishi ugenini.

Wajumbe watapata nafasi ya kuweza kupembua kazi mbali mbali zinazotekelezwa na Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki na ruzuku inayotolewa kwa Makanisa haya.







All the contents on this site are copyrighted ©.