Yaliyojiri katika kufunga Mwaka wa Imani, Jimbo kuu la Dar es Salaam
Sakramenti ya Ubatizo ni msingi wa maisha yote ya Kikristo, lango la kuingilia uzima
katika Roho. Ni mlango unomwezesha mwamini kupata Sakramenti nyingine zinazotolewa
na Mama Kanisa. Kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo, waamini wanafanywa huru toka katika
dhambi na wanazaliwa upya kwa maji na Roho Mtakatifu na hivyo kuwa ni watoto wa Mungu,
viungo hai vya Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa na wanaingizwa na kufanywa kuwa
washiriki wa maisha na utume wa Kanisa. Ubatizo ni Sakramenti ya kuzaliwa upya kwa
maji na Neno.
Maisha ya Kisakramenti yamepewa umuhimu wa pekee katika Maadhimisho
ya Mwaka wa Imani katika Majimbo mbali mbali ya Kanisa Katoliki nchini Tanzania. Katika
kuufunga rasmi Mwaka wa Imani, Jimbo kuu la Dar es Salaam, Kardinali Polycarp Pengo,
Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, amewataka waamini kusimama imara katika
imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, hata pale wanapokabiliana na magumu katika hija
ya maisha yao hapa duniani. Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka apewe kipaumbele
cha kwanza katika maisha yao.
Kardinali Pengo katika kufunga Mwaka wa Imani,
ametoa Sakramenti ya Ubatizo kwa watoto zaidi ya mia moja waliotoka katika Parokia
79 zinazounda Jimbo kuu la Dar es Salaam. Kila Parokia ilikuwa na wajibu wa kuwapeleka
watoto wawili ambao wangekuwa ni kumbu kumbu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, uliotangazwa
na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na kuendelezwa kwa kasi
na ari kubwa zaidi na Papa Francisko kwa njia ya ushuhuda wa utume na maisha yake.
Mwaka wa Imani, ilikuwa nifursa ya kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu, tayari
kuanza mchakato wa kuchuchumilia utakatifu wa maisha kwa njia ya ushuhuda wa imani
kwa Kristo na Kanisa lake. Kardinali Pengo anasema, kuna baadhi ya waamini ambao bado
wanashindwa kuimwilisha imani yao katika matendo, kwa kukiishi kile wanachoungama
katika Kanuni ya Imani, kile wanachoadhimisha katika Liturujia na Sakramenti za Kanisa;
kile wanachojitahidi kukiishi kwa kuongozwa na Amri kumi za Mungu kama dira na mwongozo
wa maisha adili na hatimaye, kile wanachokisali na kukimwilisha katika matendo ya
huruma.
Kardinali Pengo amewataka waamini Jimbo kuu la Dar es Salaam, kuishi
kikamilifu wito na dhamana yao kama Wafuasi wa Kristo kwa kutenda yale yanayo mpendeza
Mungu na mwanadamu. Katika Ibada hii ya Misa Takatifu, Jimbo kuu la Dar Es Salaam,
limezindua Kitabu cha Katekisimu ya Kanisa Katoliki, mwaliko wa kuendeleza kuyakiri,
adhimisha, ishi na kusali yale yote waliojipatia wakati wa Maadhimisho ya Mwaka wa
Imani.
Kardinali Pengo anasema, kufungwa kwa Mwaka wa Imani Jimbo kuu la Dar
es Salaam ni mwanzo wa mchakato wa kuimwilisha Imani katika matendo, kwani kila Mwaka
ni Mwaka wa Imani, kwa kuendeleza mema na mazuri waliyokirimiwa na Mwenyezi Mungu
hata pasipo na mastahili yao. Mwaka wa Imani umekuwa na mafanikio makubwa kwa waamini
Jimbo kuu la Dar es Salaam.